TUNDU Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ametetea uamuzi wa Freeman Mbowe, ‘kuomba maridhiano’ na Rais John Magufuli. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Lissu amesema, wanaompopoa Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa, kutokana na kuomba maridhiano, sio sawa na kwamba, hatua hiyo haiakisi udhaifu.
“Kutaka maridhiano sio udhaifu na sio ‘kuunga mkono juhudi.’ Kuunga mkono juhudi ni ku-surrender (kukubali matokeo), sio ku-compromise (kukubaliana/kuelewana).
“Maridhiano ni compromise, you win some you lose some (kukubaliana kushinda sehemu na kupoteza sehemu)“ ameandika Lissu kwenye ukurasa wake wa twitter.
Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa Tanganyika, tarehe 9 Desemba 2019 jijini Mwanza, Mbowe alimwomba Rais Magufuli, kutengeneza maridhiano ya kitaifa, ili kuweza kulikwamua taifa.
“Nimekuja kushiriki, kama uthibitisho wa ulazima kuwepo maridhiano, upendo na mshikamano kwa taifa letu. Tuvumiliane, tukosoane na turuhusu demokrasia; rais una nafasi ya kipekee kujenga maridhiano katika taifa,” alisema Mbowe.
Baadhi ya wanasiasa na wanaharakati walitafsiri kauli hiyo kwamba, Mbowe ameelemewa na sasa amekosa njia ya kupenya mpaka kuamua ’kuungama.’
Akizungumzia mawazo hayo, Lissu amesisitiza, kwamba suala la maridhiano sio suala la siku moja na kuwa, linachukua muda.
“ Maridhiano sio tukio la siku moja kama la jana; ni mchakato unaochukua muda kwa kutegemea mambo mbali mbali. Inawezekana jana ni mwanzo tu wa safari; lakini tunaizungumzia kama ndio mwisho.
“Nelson Mandela hakuanza kuzungumza na makaburu baada ya kutoka gerezani mwaka ’90. Mazungumzo yalianza muda mrefu akiwa bado gerezani na vita ya ukombozi ikiwa inaendelea. Na Mzee Jomo Kenyatta na wengine wengi hivyo hivyo,” ameandika Lissu.
Leave a comment