MAHAKAMA Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, imekubali ombi la wabunge viti maalum 19, kuwahoji baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), dhidi ya hati ya kiapo kinzani waliyowasilisha katika kesi waliyofungua kupinga kuvuliwa uanachama wa chama hicho. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ombi hilo liliwasilishwa na wakili wa wabunge hao, Ipilinga Panya, leo tarehe 6 Machi 2023, mahakamani hapo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha.
Hatua hiyo ni baada ya mawakili wa Chadema kuomba kufunga maswali ya dodoso waliyopanga kuwauliza wabunge watatu waliosalia, Halima Mdee, Ester Bulaya na Esther Matiko. Awali, waliwahoji maswali hayo wabunge watano, akiwemo Nusrat Hanje, dhidi ya malalamiko yao ya kufukuzwa Chadema kinyume cha sheria.
Akiwasilisha ombi hilo, Wakili Panya aliwataja wajumbe wa bodi ambao ni, Dk. Azaveli Lwaitama, Ruth Mollel, Mary Joackim, Francis Mushi, Maulidah Anna Komu na Ahmed Rashid Hamis.
Jaji Mkeha alikubali ombi hilo, na kupanga tarehe 9 Machi 2023, vigogo hao wa Chadema waanze kuhojiwa .
Wajumbe watakaoanza kuhojiwa ni Dk. Lwaitama na Mollel.
Mdee na wenzake walifungua kesi hiyo Na. 36/2022, mahakamani hapo kupinga uamuzi wa Chadema kuwavua uanachama, wakidai kwamba ulikuwa kinyume cha sheria kwa kuwa ulikuwa wa upendeleo na hawakupewa nafasi ya kusikilizwa.
Walifungua kesi hiyo baada ya Baraza Kuu la Chadema, mwaka jana kutupilia mbali rufaa zao za kupinga kufukuzwa Chadema.
Walifukuzwa Chadema mwishoni mwa 2021, kwa kosa la kukubali kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalum, bila baraka za chama hicho.
Leave a comment