RAIS wa Awamu ya Nne wa Tanzania, Jakaya Kikwete, ameishauri Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, ijikite katika kutoa elimu kwa Watanzania, juu ya fursa zilizopo kwenye Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Anaripoti Bupe Mwakiteleko, Dar es Salaam…(endelea).
Kikwete ametoa wito huo leo Ijumaa, tarehe 21 Mei 2021, katika kongamano la maadhimisho ya miaka 40 ya SADC, lililofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), mkoani Dar es Salaam.
“Wananchi wanatakiwa kuelimishwa vya kutosha ili waifahamu SADC vizuri, wajue fursa ziliopo kwa namna gani wananufaika nazo. Nadhani hili ni moja ya jukumu la uongozi uliokuwepo, pia kutengeneza mazingira yanayowezesha watu kushiriki vizuri katika fursa hizo,” amesema Kikwete.
Mkuu huyo wa UDSM amesema, SADC ina manufaa na mchango mkubwa katika kukuza maendeleo na uchumi wa Watanzania, hasa kwenye fursa za kibiashara kwani jumuiya hiyo ina mtaji mkubwa wa soko la biashara, ambapo ina watu takribani milioni 350.
“Tutengeneze namna ya kuelimisha vijana wa shule na vyuo ili waelewe SADC ni nini na imetokea wapi, shabaha zake ni zipi. SADC manufaa yake makubwa ikiwemo ya ushirikiano wa kikanda kwenye soko la bidhaa, ni soko kubwa limetengeneza watu milioni 350,” amesema Kikwete.
Mwanasiasa huyo ameshauri majukwaa mbalimbali ya vijana yaanzishwe, kwa ajili ya kujadili namna watakavyotumia fursa za kiuchumi za SADC.
“Nadhani suala kubwa ni namna gani ya kushirikisha vijana kwenye maeneo mengi, wakati umefika kutengeneza forums (majukwaa) na mabunge ya vijana ya SADC. Tunatakiwa kuwekeza kwa vijana ambao kesho na kesho kutwa watakuja kuwa viongozi wa SADC,” amesema Kikwete.
Leave a comment