ZITTO Kabwe, Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo ameungana na serikali dhidi ya Dezydelius Mgoya (mkulima), aliyefungua kesi ya kikatiba kupinga ibara ya 40 (2). Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
“Tunalinda ukuu wa Katiba, kuhusu ukomo wa Rais wa Jamhuri uwepo kama kawaida,” amesema Zitto.
Kwenye kesi hiyo, iliyopo katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, mkulima ameitaka mahakama kuondoa ibara hiyo ili rais aweze kugombea zaidi ya awamu mbili, na akishinda aruhusiwe kuongoza nchi.
“Wajibu wa chama cha siasa ni kuhakikisha kuwa tunalinda Katiba, kesi hii ya mkulima inaweza kuleta shida ya kikatiba …, ukomo wa mtu anayetumika urais wa Tanzania uendelee kama ilivyotamkwa katika Katiba,” amesema Zitto nje ya Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam.
Pia ACT-Wazalendo kupitia bodi yake ya wadhamini, kimeomba kuunganishwa kwenye kesi hiyo kuwa sehemu ya wajibu maombi dhidi ya mkulima.
Kwenye kesi hiyo iliyopo mbele ya Jaji Benhajj Masoud, mkulima amemshitaki Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo ACT-Wazalendo kupitia wakili wake Jebra Kambole, kimeomba kuunganishwa na kuwa mshitakiwa wa pili.
Leo tarehe 2 Oktoba 2019, Jaji Masoud amesema, kama ACT-Wazalendo wanataka kuwa sehemu ya wajibu maombi, wanapaswa kumwandikia mkulima barua kupitia magazeti mawili yanayosomwa kwa kiwango kikubwa nchini ili kumjulisha.
Jaji Masoud ameeleza kuwa, kesi hiyo itaendelea tarehe 10 Oktoba 2019, na kwamba mlalamikaji (mkulima) anatakiwa kufika mahakamani hapo.
Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo akiwa nje ya mahakama hiyo, amesema wameomba kuunganishwa kwenye kesi hiyo kwa kuwa, wana maslahi nayo kikatiba.
Leave a comment