GHARAMA za ujenzi wa Daraja la Mto Buhu (Munguri B), lililopo Kondoa, mkoani Dodoma, zitaingizwa katika bajeti ya Mwaka wa Fedha 2021/22. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Ni kauli ya Mwita Waitara, Naibu wa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, aliyoitoa leo tarehe 3 Mei 2021, jijini Dodoma wakati akijibu swali la Ally Makoa, Mbunge wa Kondoa mjini (CCM).
Makoa alitaka kujua, kwamba lini serikali itaanza kujenga daraja hilo ili wananchi wa upande wa pili wa mto waweze kuvuka na kupata huduma mbalimbali za kijamii upande mwingine.
“Kwa kutambua changamoto hii, wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), imetenga fedha katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/21 kwa ajili ya kufanya usanifu wa Daraja jipya katika Mto Bubu,” amesema Waitara.
Amefafanua, daraja hilo lipo katika Barabara ya Kondoa – Nunguri – Mtiriangwi – Gisambalang – Nangwa, lenye jumla ya urefu wa Km 81.4 na kwamba, barabara hiyo inaunganisha Mkoa wa Dodoma na Manyara kupitia Wilaya za Kondoa na Hanang’.
“Mvua kubwa zilizonyesha mwaka 2019/20, zilisababisha Mto Bubu kutanuka na kufanya Daraja la Munguri B kutopitika wakati wa mvua.
“Taratibu za ununuzi wa kumpata Mhandisi Mshauri zipo katika hatua za mwisho ambapo kazi hiyo inatarajiwa kuanza Juni, 2021,” amesema.
Amesema, katika mapendekezo ya bajeti ya mwaka wa fedha 2021/22, daraja hili limetengewa Sh. 66 milioni kwa ajili ya kukamilisha kazi ya usanifu, na baada ya usanifu kukamilika, ujenzi wa daraja hilo utaanza kulingana na upatikanaji wa fedha.
Leave a comment