SERIKALI ya Tanzania, imetenga Sh. 250 milioni kwa ajili ya kukamilisha maboma matano ya Zahanati ya Minyeye, Mnung’una na Msikii katika Wilaya ya Singida, Anaripoti Jemima Samwel DMC …(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumatatu Tarehe 3 Mei 2021, na Dk. Festo Dugange, Naibu Waziri Ofisi ya Rais katika kipindi cha maswali na majibu bungeni, jijini Dodoma wakati akijibu swali la Abeid Ramadhani, Mbunge Singida Kaskazini (CCM).
“Je, ni lini serikali itamaliza ujenzi wa maboma ya Vituo vya Afya yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi katika Kata za Makuro na Ngimu?” amehoji.
Akijibu swali hilo, Dk. Dugange amesema, ili kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida, katika mwaka wa fedha 2018/19 serikali iliipatia wilaya hiyo Sh. 1.5 Bilioni kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya halmashauri.
“Katika mwaka wa fedha 2020/21, hospitali hiyo ilitengewa Sh. 500 Milioni kwa ajili yaujenzi wa wodi tatu na Sh. 500 Milioni kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.”
“Pia, katika mwaka wa fedha 2021/22 serikali imetenga Sh. 250 Milioni kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati ya Minyeye, Mnung’una na Msikii katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida,” ameeleza Kandege.
Amesema, serikali itaendelea kujenga, kukarabati, kupanua na kukamilisha maboma ya miundombinu ya kutolea huduma za afya nchini yakiwamo maboma ya vituo vya afya katika Kata za Makuro na Ngimu, kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
Leave a comment