UZEMBE na kubebana ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ndio unakibomoa chama hicho kwa kiwango kikubwa. Anaripori Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
David Kafulila, Katibu Tawala wa Mkoa wa Songwe na mbunge wa zamani wa Kigoma Kusini kupitia Chama cha NCCR-Mageuzi amesema, Chadema inateswa na umimi hivyo, kusababisha makada wake kukihama na kuingia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Uzembe na kubebana ndio siri ya wanasiasa wengi kuamua kuhama na kujiunga CCM. Haya ndio waliyakimbia CCM huko nyuma, sasa yanatokea Chadema,” ameeleza Kafulila na kuongeza;
“Kukimbilia CCM ni matokeo ya mapinduzi makubwa ya kimwenendo ndani ya CCM kama jina lake linavyosadifu. Uwezo mkubwa wa CCM chini ya uenyekiti wa Rais Magufuli kutekeleza mkakati wa kujivua gamba la ufisadi. “
Kafulila ambaye aliwahi kuwa mwanachama wa Chadema na baadaye kutimkia NCCR Mageuzi na kushinda ubunge kupitia chama hicho mwaka 2010, amesema wanasiasa wa Chadema wamechoshwa na viongozi wao.
“Watu wanaweza kwenda CCM kwa sababu wanavutiwa na CCM au wamechoshwa na upinzani. Kwa nionavyo mimi, watu wengi wanajiunga CCM kwa kuvutiwa na CCM kutokana na ukarabati mkubwa wa CCM na Serikali yake uliofanywa na Rais Magufuli ndani ya muda mfupi,” amesema.
Leave a comment