Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa chama cha ACT Wazalendo, Janeth Rithe ametangaza rasmi kugombea nafasi ya Uenyekiti wa Ngome ya Wanawake Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari iliyotolewa leo tarehe 9 Februari 2024; amesema anagombea nafasi hiyo akiamini anao uwezo, uthubutu na uimara kuongoza ngome hiyo.
Rithe ambaye amekuwa mwenezi wa chama hicho kwa mafanikio makubwa amewaasa wanachama na wanawake wa ACT Wazalendo kwamba hawatojuta endapo watampa ridhaa ya kuongoza Ngome hiyo.
“Nitagombea nafasi ya Uenyekiti wa Ngome ya Wanawake Taifa wa chama chetu katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika tarehe 2 Machi 2024.
“Ninagombea nafasi hii nikijua kabisa kwamba Ngome ya Wanawake inahitaji kiongozi mwenye uthubutu, imara, shupavu na mwenye ushawishi wa kuweza kuunganisha nguvu ya wanawake ndani na nje ya chama kwa maslahi mapana ya Taifa kwa ujumla.
“Niwahakikishie wanawake wa ACT Wazalendo na wanachama kwa ujumla kwamba ninagombea nafasi hii nikiamini ninazo sifa hizo. Hivyo hawatojuta endapo watanipa ridhaa ya kuongoza Ngome ya Wanawake.” amesema Rithe.
Aidha, kupitia taarifa hiyo; Rithe amewaalika waandishi wa habari kuhudhuria mdahalo wa wagombea wa nafasi za Ngome ya Wanawake utakaofanyika tarehe 24 Februari 2024.
Leave a comment