JAJI Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma, amekitaka Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), kuwafikisha mbele ya kamati ya maadili wanachama wake watakaobainika kwenda kinyume na maadili ya taaluma hiyo, badala ya kusubiri majaji kuchukua hatua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Prof. Ibrahim ametoa agizo hilo leo tarehe 1 Desemba 2023, baada ya kuwapokea na kuwakubali mawakili wapya 279, siku chache baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya Mawakili, Jaji Ntemi Kilikamajenga, kumsimamisha uwakili kwa muda wa miezi sita, Mpale Mpoki, akituhumiwa kukiuka maadili ya taaluma hiyo.
Mpoki ambaye ni wakili mwandamizi mwenye uzoefu wa miaka 34, inadaiwa alipewa adhabu hiyo baada ya kutangaza nia ya kukata rufaa juu ya uamuzi mdogo uliotolewa na kamati hiyo, dhidi ya mteja wake, Wakili Boniface Mwabukusi, aliyeshtakiwa kwa ukiukwaji wa maadili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Kiongozi huyo wa mahakama, amesema amepokea malalamiko mengi kutoka kwa baadhi ya majaji kuhusu lugha ambazo baadhi ya mawakili wanatumia mahakamani, ambazo zinaonyesha jeuri, dhihaka na dharau dhidi yao, kinyume na kanuni ya 92 ya kanuni za maadili ya mawakili.
“Naomba kukitokea tukio kama hilo isiwe jaji ndiyo alalamike, mawakili ndiyo wa kuchukua jukumu la kulalamika na kupeleka kwenye vyombo vyenu kwamba wakili mwenzetu amevunja heshima mbele ya mahakama na sisi TLS sababu tunataka kulinda taaluma yetu tunamfikisha kwenye baraza watamsikiliza baadae watatoa adhabu,” amesema Prof. Juma.
Prof. Juma amesema hata katika nchi ambazo Tanzania imeiga mifumo yake ya kisheria, ikiwemo Uingereza, mamlaka za nikinidhamu huwachukulia hatua mawakili hata kama ni waandamizi, ambao wanaonyesha dharau kwa majaji wakati wa usikilizaji kesi.
Kuhusu mawakili wapya, Prof. Juma amewataka kutowaiga mawakili wanaokiuka maadili kwenye utekelezaji wa majukumu yao, bali wawaige wale wanaozingatia maadili na kuiheshimu mahakama.
Leave a comment