RAIS Samia Suluhu Hassan amesema ujenzi wa Ikulu ya Rais inayojengwa katika makao makuu ya nchi Chamwino jijini Dodoma umefikia asilimia 75. Anaripoti Helena Mkonyi, TUDARCo … (endelea).
Amesema ujenzi huo ni mwendelezo wa utekelezaji wa dhamira ya serikali kuhamia jijini Dodoma.
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 14 Septemba 2021 wakati akizindua kitabu cha mkakati wa uelimishaji na uhamasishaji wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022.
Amesema mipango ya serikali ya kulifanya jiji la Dodoma kuwa jiji la kisasa upo palepale.
“Hivi karibuni Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alikagua ujenzi wa ikulu mpya na sasa umefikia asilimia 75.
“Ujenzi wa kiwanja kikubwa cha ndege cha kimaitaifa utaanza hivi karibuni kwani jana mkataba wa ujenzi huo umesainiwa.
“Ujenzi wa majengo mji wa kiserikali kule Mtumba unaendelea, kutajengwa majengo makubwa ya ghorofa kutegemea na pesa ambazo kila wizara itapewa.
“Kuhusu miundombinu tayari tumesaini ujenzi wa barabara ya mzunguko ambayo ujenzi wake ulicheleweshwa kwa sababu ya taratibu za fidia lakini sasa muda si mrefu utaanza,” amesema.
Aidha, amesema serikali imeendelea kuboresha huduma za matibabu ya kibingwa katika hospitali ya mkoa na ile ya Benjamini Mkapa.
“Pia Serikali tumetoa kiasi cha Sh bilioni 17.9 kwa jili ya ujenzi wa Chuo kikubwa cha Ufundi Stad (VETA) – Dodoma kule Nala. Ujenzi huo utakamilika hivi karibuni na chuo kitaanza na udahili wa wanafunzi 1500 lakini baadae watafikia 5000.
“Kwa kuwa changamoto kubwa hapa Dodoma ni upatikanaji wa maji, Serikali imejipanga kutekeleza mradi mkubwa wa bwawa la Farkwa ili kumaliza kabisa tatizo hilo la upatikanaji wa maji,” amesema.
Story inahusu Ikulu lakini picha ni ya mji wa Dodoma. Hamkuweza kupata picha ya hiyo Ikulu? Tumieni weledi wa uandishi !!