SPIKA wa Bunge la Tanzania, Dk. Tulia Ackson, amewataka wabunge tisa wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA), kusimamia maslahi ya Tanzania pamoja na kuwasilisha hoja za nchi badala ya hoja zao binafsi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Spika Tulia ametoa agizo hilo leo Alhamisi, tarehe 22 Septemba 2022, bungeni jijini Dodoma, muda mfupi baada ya Katibu wa Bunge, Nenelwa Mwihambi, kuwatangaza washindi wa uchaguzi wa EALA.
“Wabunge hawa ndiyo wabunge tumewachagua sisi siku ya leo kwa niaba ya wananchi wote kwenda kutuwakilisha kama Tanzania kwenye Bunge la Afrika Mashariki na tunawategemea mnapokwenda kule si hoja ya mawazo yenu, ni hoja ya nchi inasemaje na tunaamini mtaenda kusimamia maslahi ya nchi kama mlivyoahidi hapa,” amesema Spika Tulia.
Aidha, Spika Tulia amewataka wabunge hao wateule kuzingatia majukumu yao watakayopewa na EALA, pamoja na kutoa mrejesho kwa Bunge la Tanzania juu ya kazi watakazozifanya.
“Niwape ushauri kama ambavyo sisi huwa tunaenda majimboni kwetu, ninyi jimbo lenu ni hili hapa kwa niaba ya Watanzania. Lakini muhimu kuzingatia kazi zile ambazo mnapaswa kuzifanya huko, huku lazima mtupatie taarifa kwa kazi zenu kwa kadiri ambayo mnatakiwa kufanya hivyo na kanuni,” amesema Spika Tulia.
Wabunge hao wateule ni Angella Kiziga, aliyepata kura 322, zilizopigwa katika kundi la wagombea wanawake, mwingine katika kundi hilo ni Nadra Juma Mohammed (310), Dk. Shogo Mlozi (322).
Wabunge waliochaguliwa kutoka kundi la wagombea kutoka Zanzibar, ni Abdullah Makame aliyepata kura 305, kati ya kura 311 zilizopigwa na Machano Ally Machano (291).
Mashaka Ngole, kutoka Chama cha Wananchi (CUF), amechaguliwa katika kundi la wagombea wa vyama vya waliowachache bungeni, ambapo amepata kura 234, kati ya kura 319 zilizopigwa.
Kwa upande wa kundi la wagombea wa Tanzania Bara, walioshinda ni Ansar Abubakar Kachwamba, aliyepata kura 300 kati ya kura 313 zilizopigwa. Wengine ni James Kinyasi Millya (312) na Dk. Ngwalu Jumanne Maghembe (311).
Leave a comment