MKURUGENZI mpya wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Keneth Weston, amefanya mazungumzo na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania, kuhusu masuala mbalimbali yenye lengo la kuimarisha tasnia hiyo nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Weston aliyechaguliwa kushika wadhifa huo Julai, 2022, amefanya mazungumzo na Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, leo Alhamisi, tarehe 22 Septemba mwaka huu, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kitengo cha habari cha THRDC, kikao hicho kimelenga kujadili namna wandishi wa habari watakavyojengewa uwezo katika kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hususan masuala ya haki za binadamu.
“Kikao hicho kimejadili mambo mbali mbali ya mashirikiano baina ya Mtandao na UTPC katika kukuza na kuendeleza tasnia ya Habari nchini, hususani kuwaendeleza kwa kuwajengea uwezo waandishi ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi huku wakizingatia misingi ya tasnia, sheria na pamoja na haki za binadamu,” imesema taarifa hiyo na kuongeza:
“Tangu kuanzishwa kwake, THRDC imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na tasnia ya Habari, hasa katika kuwajengea uwezo waandishi wa Habari katika maswala mbali mbali ya haki za binadamu, pamoja na Msaada wa dharura pindi mwandishi anapopatwa na changamoto mbali mbali katika utekelezaji wa majukumu yake.”
Leave a comment