BAADHI ya viongozi wa halmashauri za Mkoa wa Dar es Salaam, wamedai hatua ya aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli kuvunja lililokuwa jiji la Dar es Salaam, imekwamisha maendeleo na kuomba lirejeshwe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yameibuliwa leo tarehe 5 Machi 2024, katika kikao cha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa huo.
Kupitia kikao hicho, imeelezwa kuwa kitendo cha jiji hilo kuvunjwa kinapelekea viongozi wa halmashauri za Dar es Salaam, kukosa jukwaa zuri la kukutana na kupanga namna ya kuleta maendeleo ya mkoa huo, kama ilivyokuwa awali kabla ya kuvunjwa.
Kufuatia malalamiko hayo, Chalamila aliwataka waangalie namna ya kukutana mara kwa mara kuweka mikakati ya kutatua changamoto zao kwani uamuzi wa jiji hilo kuvunjwa ulitokana na mamlaka ya rais.
“Unajua jiji lilishavunjwa, kuja tena kulia kwamba hamna platform ya kujadiliana kuhusu maendeleo ya halmashauri zenu. Jiji lisiwe kisingizio cha kwamba kila tunapofeli katika mji ni kwa sababu jiji halipo, kumbukeni hakuvunja kiongozi wa kawaida lilivunjwa na mamlaka ya Rais na mamlaka ya Rais ni kitu kingine sasa nini kinachofuata hapa tunatakiwa tujadiliane,” amesema Chalamila.
Katika hatua nyingine, Chalamila alizitaka halmashauri za Dar es Salaam kuweka mipango ya kifedha kwa ajili ya kuuboresha mkoa huo ukiwemo kujenga miundombinu ya kisasa na majengo ya ghorofa.
Pia, aliwataka viongozi wa halmashauri hizo waweke mikakati itakayomaliza changamoto ya uchafu wa mazingira ndani ya Dar es Salaam.
Jiji la Dar es Salaam, lilivunjwa Februari 2021 na Rais Magufuli ambapo alipandisha hadi Halmashauti ya Manispaa ya Ilala kuwa jiji. Sababu ya uamuzi huo ilitajwa kuwa kubana matumizi ya fedha kwa kuendesha jiji ambalo lilikuwa halina vyanzo vya mapato vya kutosha.
Leave a comment