RICHARD Kapinye, diwani wa kata ya Kibaigwa na Mwenyekiti wa kamati ya uchumi, ujenzi na mazingira ya halmashauri ya Wilaya ya Kongwa ameiomba serikali ya Rais John Magufuli kuagiza chakula kwenye mfumo wa soko ili kupunguza bei ya nafaka hususan mahindi, anaandika Dany Tibason.
Kapinye alitoa kauli hiyo katika kikao cha baraza la madiwani wakati akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo.
Amesema serikali ikiingiza chakula sokoni na kuuza angalau debe kwa sh.10,000/= waliohifadhi chakula katika maghala watatoa nafaka na kuziuza kwa bei nafuu ili wananchi waweze kumudu kununua nafaka hizo.
“Bei ya mahindi kwa debe moja kwa sasa ni kati ya Sh. 20,000/= hadi 22,000/= katika maeneo mengi wilayani Kongwa na mvua imeanza wiki hii” amesema Kapinye.
Pamoja na ombi la kamati hiyo kwa serikali, Deogratias Ndejembi Mkuu wa Wilaya hiyo amesisitiza wananchi kujikita katika kilimo cha mtama na mazao mengine yanayostahimili ukame kutokana na mabadiliko ya tabia ya nchi.
Katika kikao hicho Chilingo Chimeledya, mwenyekiti wa kamati ya huduma za jamii ambaye pia ni diwani wa kata ya Sejeli alitoa shukrani kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msaada wa madawati 997 Katika halmashauri ya Kongwa.
Kamati hiyo imemshukuru Job Ndugai, Mbunge wa Jimbo la Kongwa na spika wa Bunge la Jamhuri ya muungano wa Tanzania kwa kufanikisha upatikanaji wa Dola za Kimarekani 10,000/= kutoka ubalozi wa China.
“Fedha hizo zilitumika kununua saruji mifuko 1,557 iliyogawanywa ili kukamilisha ujenzi wa madarasa ya shule yaliyo kwenye hatua mbalimbali za ukamilishaji,” amesema.
Leave a comment