Mbunge wa zamani wa Busega na rafiki wa karibu aliyekuwa Waziri Mkuu mstaafu, Hayati Edward Lowassa, Dk. Raphael Chegeni (CCM) amesema huenda mwanasiasa huyo angeishi muda mrefu kama asingepata ajali za kisiasa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mbunge huyo wa zamani, ametoa kauli hiyo leo tarehe 14 Februari 2024, akitoa salamu za pole katika ibada fupi ya kuuaga mwili wa Lowassa, iliyofanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Azania Front, jijini Dar es Salaam.
“Jana Mzee Joseph Warioba ulizungumza kile ambacho unacho moyoni, hukuongea kama wanasiasa tuliojaa lugha tofauti. Wazee kama ninyi katika taifa hili tunawahitaji sana kwa sababu tunahitaji kujenga taifa la watu wanaosema kweli.
“Ninafahamu wala sio siri – Zaburi ya 90 inaeleza kuhusu uhai wa mwanadamu miaka 70 sana sana miaka 80 lakini naamini Edward Lowassa angeweza kuishi zaidi kama isingekuwa ajali mbalimbali za kisiasa,” amesema Dk. Chegeni.
Miongoni mwa ajali za kisiasa alizowahi kupata Lowassa, ni kashfa za ufisadi zilizopelekea kujiuzulu uwaziri mkuu 2008, pamoja na kukatwa katika kura za maoni za kinyang’anyiro cha uteuzi wa mgombea urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), zaidi ya mara moja.
“Lowassa alifanya kazi kubwa, hata baada ya kupata ajali ya kisiasa alibeba mzigo usiokuwa wa kwake. Kwa heshima ya CCM na kulinda heshima yake aliamua kujiuzulu, viongozi wachache sana hasa kwa Tanzania hukubali kuachia madaraka kama alivyofanya,” amesema Dk. Chegeni.
Akizungumzia utendaji wa Lowassa, Dk. Chegeni amesema ameacha alama katika mioyo ya watanzania kwa kuwaletea maendeleo katika kipindi kifupi alipopata dhamana ya uongozi.
Leave a comment