SPIKA wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amewaapisha wabunge watatu akiwemo Dk. Bashiru Ally. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Walioapishwa ni; Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Balozi Libareta Mulamula na Dk. Bashiru.
Wabunge hao wameapishwa leo Alhamisi tarehe 01 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma baada ya jana Jumatano, kuteuliwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Kabla ya uteuzi huo, Dk. Bashiru alikuwa Katibu Mkuu Kiongozi, nafasi aliyoitumikia kwa siku 32 kuanzia tarehe 27 Februari hadi jana Jumatano.
Mbali na kumteua Balozi Mulamula kuwa mbunge, alimteua kuwa waziri wa mambo ya nje huku Balozi Mbarouk kuwa naibu waziri wa mambo ye nje.
Kabla ya uteuzi huo, Mbarouk alikuwa Balozi wa Tanzania katika Falme za Kiarabu (UAE).
Katika shughuli hiyo ya kuapishwa, Balozi Mulamula alionekana mwenye furaha tangu anaingia na kumaliza kuapishwa akicheza cheza, hali iliyowafanya wabunge kushangilia.
Mara baada ya kumaliza kuapishwa, Spika Ndugai amewapongeza wabunge hao na kuwakaribisha bungeni wabunge hao wapya.
“Mawaziri ninyi ni wabunge, mikiwa huko nje mjue nafasi yenu,” amesema Spika Ndugai
Spika Ndugai amesema, kutokana na mabadiliko yaliyofanywa ya baraza la mawaziri “leo hatukakuwa na maswali na majibu ili kutoa nafasi kwa walioteuliwa kuapishwa na kukabidhiwa ofisi.”
Leave a comment