LICHA Baraza la Mawaziri kufanyiwa mabadiliko mara kadhaa tangu mwaka 2015, mawaziri watatu na naibu waziri mmoja bado hawajaguswa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mawaziri wasioguswa katika wizara zao tangu utawala wa Rais John Magufuli mwaka 2015, ni Jenista Mhagama ambaye ni Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu,.
Wengine ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi na naibu wake, Angelina Mabula. Pamoja na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako.
Tarehe 31 Machi 2021, Rais Samia Suluhu Hassan alifanya mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri.

Kiongozi huyo mpya wa Tanzania, alitangaza mabadiliko hayo Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, katika hafla ya kumuapisha Dk. Phillip Mpango, aliyemteua kuchukua nafasi yake ya Makamu wa Rais.
Enzi za uongozi wa Dk. Magufuli alifanya mabadiliko madogo ya baraza la mawaziri zaidi ya mara mbili, ikiwemo 2015, 2019 na 2020, ambapo kuna mawaziri na naibu waziri ambao hawakuguswa, hadi katika mabadiliko yaliyofanywa jana na Rais Samia.
Katika mabadiliko ya baraza hilo, Rais Samia ameongeza naibu waziri mmoja katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, ambapo Mwanaidi Ally Hamis amekuwa Naibu Waziri anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Awali, katika wizara hiyo alikuwa Dk. Dorothy Gwajima (waziri) na Dk. Godwin Mollel (naibu waziri).
Pia, Wizara ya Uwekezaji aliitoa katika Ofisi ya Rais na kuihamishia katika Ofisi ya Waziri Mkuu.
Rais Samia ameapishwa kuchukua uongozi wan chi kufuatia kifo cha Dk. Magufuli kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Leave a comment