DENI la Serikali imeongezeka kwa takribani Sh. 11 trilioni sawa na asilimia 15, kutoka Sh. 71.31 trilioni (2021/22) hadi kufikia Sh. 82.25 trilioni (2022/23). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 28 Machi 2024, Ikulu jijini Dodoma na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, akimkabidhi ripoti za ukaguzi kwa mwaka wa fedha wa 2022/23, Rais Samia Suluhu Hassan.
“Mwenendo wa deni la serikali, kufikia tarehe 30 Juni 2023 ilikuwa trilioni 82.25 sawa na ongezeko la asilimia 15 kutoka trilioni 71.31 mwaka 2021/22. Deni hilo linalojumuisha deni la ndani la trilioni 28.92 na deni la nje ni trilioni 53.32,” amesema CAG Kichere.
CAG Kichere amesema deni hilo ni himilivu “kipimo cha deni la serikali kinachotumia pato la taifa kinaonesha deni hili ni himilivu.Hali kadhalika uwiano wa kulipa madeni na mauzo ya nje ni asilimia 12, chini ya kiwango cha ukomo cha asilimia 15 na uwiano wa malipo ya madeni na mapato ni asilimia 14.3 chini kidogo ya kiwango cha ukomo elekezi chini ya asilimia 18.”
Aidha, CAG Kichere amesema makusanyo ya kodi ya serikali yameongezeka kwa asilimia 8 hadi kufikia Sh. 22.58 trilioni (22/23), ukilinganisha na makusanyo ya Sh. 20.94 trilioni (2021/22).
Kuhusu ukaguzi uliofanywa na ofisi yake, CAG Kichere amesema amesema wametoa hati 1,209 ambapo zinazoridhisha ni 1,197, zenye shaka 9, mbaya 1 na 2 zimeshindwa kutolewa maoni.
Leave a comment