WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Ummy Mwalimu amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Gairo (DED), Mkoa wa Morogoro, Asajile Mwambambe. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Mwambambe anatakiwa kurudi Halmashauri ya Kilosa mkoani humo ili kujibu tuhuma mbalimbali zinazomkabili ikiwemo upotevu wa mabati 1,172.
Wakati upotevu huo unatokea, Mwambambe alikuwa mkurugenzi wa Kilosa kabla ya baadaye kuhamishiwa Gairo na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Tarehe 24 Agosti 2021, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Fortunatus Musilimu aliwaeleza waandishi wa habari kwamba linamshikilia Mwambambale na wenzake sita kwa tuhuma ya wizi wa mabati 1,172 yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 31.
Alisema taarifa zinaonesha fedha hizo zilitolewa na halmashauri ya Kilosa, kwa ajili ya ujenzi wa shule ya msingi ya kijiji cha Mbumi kata ya Mbumi, lakini badala yake zilirudishwa kwa mbinu za ujanjaujanja.
Kamanda Musilimu alisema Juni 17 mwaka huu, kuliripotiwa tukio la wizi wa mabati yaliyohifadhiwa kwenye ghala la halmashauri ya Kilosa, na baada ya uchunguzi ilibainika hakukuwa na viashiria vyovyote vya kuvunjwa kufuli kwenye ghala hilo wala milango kubomolewa.
Leo Ijumaa, tarehe 10 Septemba 2021, Nteghenjwa Hoseah, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Tamisemi amesema, Waziri Mwalimu amemsimamisha kazi Mwambambwe ili arudi Kilosa kujibu tuhuma hizo.
Taarifa hiyo imesema, mabati hayo yamkwisha kupatikana na kurejeshwa eneo husika kuendelea na kazi iliyokuwa imekusudiwa.
Katika taarifa hiyo, imemnukuu Waziri Umma akiwataka watumishi wa wote wa umma kufanya kazi kwa weledi, kuwa waadilifu na makini katika utendaji kazi wao wa kila siku.
Leave a comment