CHAMA cha siasa nchini Tanzania- Chama Cha Wananchi (CUF) kimempongeza Msajili wa vyama vya siasa nchini humo, Jaji Francis Mutungi kwa kuandaa mkutano baina ya wadau wa vyama vya siasa na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya leo asubuhi Jumatatu, tarehe 6 Septemba 2021, Jaji Mutungi kuviomba vyama vya siasa kusitisha mikutano na makongamano ili kusubiri kikao hicho baina yao na IGP Sirro kitakachofanyika hivi karibuni.
Taarifa ya Mhandisi Mohamed Ngulangwa, Mkurugenzi wa Habari Uenezi na Mahusiano na Umma wa CUF amesema, uamuzi wa Jaji Mutungi wa kuona umuhimu wa kukutanisha wadau wa siasa nchini lina jambo zuri kwa mustakabli wa demokrasia nchini.
“Ni matumaini yetu kikao hicho muhimu baina ya msajili, viongozi wakuu wa vyama vya Siasa na Jeshi la Polisi kitafanyika haraka iwezekanavyo na hatimaye ile kauli ya Msajili ambayo hakupenda kuitafsiri kwamba Tanzania “si Military State” ikaanza kutafsirika kivitendo, kama moja ya matunda yanayotarajiwa,” amesema MHandisi Ngulangwa.
Amesema “bila shaka kikao hicho pia kitawaacha huru wale wote wanaosota kwa kesi mbalimbali za kubambikwa ambazo kiini chake ni harakati za kisiasa.”
Hata hivyo, chama hicho kimesikitishwa na kauli ya msajili ya kuvitaka vyama vya siasa kusimamisha makongamano na mikutano ya hadhara mpaka kifanyike kikao hicho ambacho hakijapangiwa tarehe.
“Kwa nafasi yake kama mlezi wa vyama, msajili alitarajiwa kutoa ufafanuzi wa sheria mbalimbali ili kulielimisha Jeshi la Polisi kwamba mikutano ya hadhara na makongamano ni ruhusa ya kisheria kwa vyama vyote, si CCM pekee,” amesema
Leave a comment