HOSPITALI ya Taifa ya Muhimbili (MNH)- Upanga na Mlonganzila, Mkoa wa Dar es Salaam, imeweka sharti kwa wananchi, wafanyakazi na wanafunzi wanaokuwa maeneo ya hospitali hiyo, kuvaa barakoa wakati wote. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Lengo ni kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19).
Sharti hilo, limetolewa leo Jumanne, tarehe 22 Juni 2021 na Aminiel Aligaesha likiwa na lengo la kuhakikisha kila mmoja anachukua tahadhari ya kujikinga na kuwakinga wengine kuhusu corona.
“Kuvaa barakoa wakati wote wanapokuwa katika mazingira ya hospitali. Hakuna atakayeruhusiwa kuingia ndani ya eneo la hospitali bila kuvaa barakoa.
“Wafanyakazi wote na wanafunzi kuanzia sasa, wanapaswa kuvaa barakoa wakati wote wakiwa mazingira ya kazi. Hakuna mfanyakazi au mwanafunzi atakayeruhisiwa kutoa huduma kwa mgonjwa bila barakoa kuanzia kliniki, kwenye vipimo au wodini,” amesema Aminiel.
Aminiel amesema, watu wote wanaoingia maeneo ya hospitali, watapaswa kunawa mikono kwa kutumia sabuni na maji tiririka yaliyopo katika maeneo mbalimbali ya hospitali au vipukusi ‘sanitizer.’
“Eneo la Muhimbili lina msongamano, hivyo tunashauri idadi ya wasindikizaji kwa wagonjwa wanaokuja kliniki nayo kupungua hivyo mgonjwa ataruhusiwa kuja na msindikizaji mmoja,” amesema Aminiel na kuongeza:
“Wagonjwa waliolazwa wodini, wataruhusiwa kuonana na ndugu zao watano tu kwa siku ambapo asubuhi ni ndugu wawili, mchana mmoja na jioni wawili.”
Leave a comment