BAADA ya Baraza la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha), kuanza harakati za kudai katiba mpya, Baraza la Wanawake la chama hicho (Bawacha), nalo limeanza kusaka tume huru ya uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Chadema kimegawa majukumu ya utafutaji katiba mpya na tume huru ya uchaguzi, kwa mabaraza yak. Bavicha lililokabidhiwa jukumu la kutafuta katiba mpya, lilianza safari hiyo Julai Mosi 2021, baada ya kufungua kongamano la katiba mpya, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na wanachama wa Chadema, jana tarehe 4 Julai 2021, mkoani Dar es Salaam, Kaimu Mwenyekiti wa Bawacha Taifa, Sharifa Suleiman, alisema watafanya kazi usiku na mchana kudai tume huru ya uchaguzi.
https://www.youtube.com/watch?v=jFxNnASPKzY
Kaimu Mwenyekiti huyo wa Bawacha alisema, tume huru ya uchaguzi ndiyo itakawezesha chaguzi kuwa za huru na za haki.
“Bawacha tumepewa kazi kubwa ya kudai tume huru, wakati vijana wao wamepewa katiba mpya. Tume huru tunalazimika kuidai asubuhi, mchana na jioni. Ndiyo itakayowezesha kupata haki katika uchaguzi wetu wa 2025. Bila tume huru hatutaweza kufanikiwa na hatutaweza kuwa na uchaguzi halali,” alisema Sharifa.
Sharifa aliwaomba wafuasi wa Chadema kuweka tofauti zao pembeni, ili wajumuike pamoja katika kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi.
“Naomba sana kina baba na vijana tushirikiane kwa pamoja kudai tume huru na katiba mpya, muda ni huu sasa,” alisema Sharifa na kuongeza:
“ Tuweke tofauti zetu pembeni sababu hatutaweza kufika kule tunakotaka ikiwa sisi wenyewe hatuko vizuri ndani ya chama chetu. Umoja, ushirikiano, upendo ndiyo nguzo kuu ya kutupeleka katika azma na lengo letu.”
Chadema kimeweka msimamo wa kutoshiriki chaguzi, hadi tume huru ya uchaguzi itakapopatikana, kwa madai kwamba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), haiko huru.
Hata hivyo, tume hiyo mara kadhaa imepingana na madai hayo, ikisema inaendesha shughuli zake kwa mujibu wa sheria.
Tangu kiliposhiriki Uchaguzi Mkuu wa 2020, kisha kukataa matokeo yake, Chadema kimesusa kushiriki chaguzi kadhaa ndogo, ikiwemo za majimbo ya Buhigwe na Muhambwe, mkoani Kigoma.
Katika uchaguzi huo, Chama Cha Mapinduzi kilipata ushindi wa zaidi ya asilimia 90, kwa kupata wabunge wa majimbo na viti maalumu zaidi ya 300.
Huku wa vyama vya upinzani vikiwa na wabunge 24, wanne wa majimbo, wanne wa ACT-Wazalendo na mmoja wa Chama cha Wananchi (CUF). Pamoja na 19 wa viti maalumu, ambao walivuliwa uanachama wa Chadema.
Mbali na Chadema, CUF nacho kimesusa kushiriki chaguzi, hadi tume huru itakapopatikana, wakati ACT-Wazalendo kikishiriki kwa maelezo kwamba , kinapima uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Vizuri sana lakini ukumbuke wale walio taka kuibadirisha katiba ya chadema walifukuzwa hapo chadema kwa io kwanza tuibadirishe katiba yetu chadema ambayo inamfanya mwenye kiti wa chadema kuwa wa kudumu