CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imesema Kikosi Kazi cha kuratibu maoni ya kuimarisha demokrasia ya vyama vingi cha Rais Samia Suluhu, ilikuwa mbinu ya kuchelewesha mchakato wa katiba mpya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Akizungumza katika mkutano mkuu maalum wa Majimbo ya Nyamagana na Ilemela jijini Mwanza, jana tarehe 29 Desemba 2022, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, alidai kila mtu alipozungumza kuhusu ukamilishaji mchakato wa upatikanaji katiba mpya, aliambiwa asubiri matokeo ya utekelezaji wa mapendekezo ya kikosi hicho.
“Watawala ili kuvuta muda na kupata kisingizio cha kuvuta muda wakaanzisha kitu kingine kikosi kazi cha rais, ikawa yeyote akizungumza mabadiliko na maboresho ya katiba, sheria na haki anaambiwa subiri matokeo ya ripoti ya kikosi kazi na baadhi wakaingia mtego wakawa na matumaini kwamba Chadema wamegoma kuingia kikosi kazi hawataki mazungumzo,”
“Hawa wanajipenda wenyewe, kumbe Chadema tuliona kuanzia mwanzo kwamba hakuna cha maana kitakachotokana na kikosi kazi, isipokuwa kuchelewesha muda wa mabadiliko katika taifa letu,” alisema Mnyika.
Mnyika alisema kuwa, kama muswada wa kurejesha, kuendeleza na kukamilisha mchakato wa katiba mpya hautapelekwa bungeni Februari 2023, haitapatikana kabla ya chaguzi zijazo, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025.
“Kama muswada huo usipoingia bungeni Februari 2023, uwezekano wa katiba mpya kukamilika na kutumika kwa ajili ya chaguzi zijazo itakuwa sawa sawa na ngamia kupenya kwenye tundu la sindano sababu hakutakuwa na bajeti ya kufanikisha mchakato huo,” alisema Mnyika.
Kikosi kazi hicho kiliundwa na Rais Samia kwa ajili ya kufanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na wadau kwa ajili ya kuimarisha demokrasia ya vyama vingi, ambapo kilipendekeza mchakato wa katiba mpya uanze baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2025.
Leave a comment