MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, amesema Tanzania iko katika zama nzuri kutokana na kuwepo kwa uhuru wa habari uliyoyumba miaka sita iliyopita.Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Balile ametoa kauli hiyo jana tarehe 29 Desemba 2022, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam, katika hafla ya utoaji tuzo za wanahabari waliofanya vizuri kwenye kuripoti habari za watoto na ugonjwa wa Virusi vya Korona ulioibuka 2019 (UVIKO-19).
Balile alisema, zama hizi ni nzuri kwa kuwa kuna dalili za sheria zinazokandamiza uhuru wa habari kurekebishwa, ili ziwe rafiki.
“Wote tunafahamu miaka sita iliyopita kipindi tulichopitia, kwahiyo watu hawajaamini kwamba uhusu wa habari ni suala la msingi. Naweza kusema zama tulizopo sasa ni nzuri ukilinganisha na tulikotokea na kuna dalili sheria hizi zitabadilishwa kama ambavyo tumekubaliana kwenye vikao viwili kati ya wadau wa habari na Serikali,” alisema Balile.
Balile alisema, Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na makamu wake, Dk. Phillip Mpango, sambamba na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wamekuwa waumini wa kweli wa uhuru wa vyombo vya habari.
“Ukiona Rais ni muumini wa vyombo vya habari, makamu wa Rais mliona kwenye kongamano la wanahabari Iringa na akatamka kabisa kwamba vyombo vya habari ni mmhimili wan ne wa dola akasema tusimame tuhakikishe mambo yanakwenda vizuri. Waziri Mkuu ndiyo usiseme ametuchagiza tufanye habari za uchunguzi ili kuibua yale yaliyofichika,” alisema Balile.
Balile alisema, marekebisho ya sheria za habari yakikamilika Tanzania itakuwa na sheria nzuri ambapo nchi jirani zitakuja kujifunza.
Mwenyekiti huyo wa TEF alisema, kwa sasa Serikali ina mpango wa kuwasilisha bungeni jijini Dodoma, Muswada wa marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, ifikapo Januari 2023, kisha baada ya hatua hiyo itakutana na wadau kujadili namna ya kuifanyia maboresho Sera ya Habari na Utangazaji ya 2003, ili iende na wakati pamoja na kuondoa mapungu yake.
Leave a comment