CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Songwe kimeitaka Wizara ya Ujenzi kufanya juu chini kwa kutekeleza ujenzi wa barabara za maeneo matatu zinazokera zaidi mkoani humo ili kupunguza changamoto za wananchi. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe … (endelea).
Katibu wa CCM mkoa huo, Said King’eng’ena amesema hayo mbele ya Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya aliyefika ofisi ya CCM mkoa Oktoba 6- 2023 akiwa katika ziara yake mkoani humo kukagua barabara zinazosimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).
King’eng’ena ametaja barabara ambazo wakazi wa Songwe wana hamu zijengwe kwa lami kuwa ni ya kutoka Mlowo hadi Kamsamba huku akisema itapendeza zaidi ikijengwa barabara yote na kwa kipindi hiki.
Amesema barabara nyingine kero kwa Wanasongwe ni ya kutoka Mbeya hadi Tunduma na kwamba watu wanaisubiri kwa hamu ili ijengwe kipindi hiki kupunguza ajali.
Aidha amesema kero nyingine kwa Mkoa wa Songwe ni ubovu wa barabara za Mitaa ya Mji wa Vwawa ambao ni makao makuu ya Mkoa wa Songwe.
Amemtaka Naibu Waziri huyo akakutane na maofisa wa TARURA ili waboreshe barabara za Mitaa ya Vwawa akisema kwa sasa zinatia aibu.
Akizungumza kwa kujibu, Mhandisi Kasekenya amesema Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuboresha barabara zote nchini zikiwamo za Mkoa wa Songwe.
Amesema maandalizi ya ujenzi wa barabara kutoka Igawa hadi Tunduma yanaendelea na kwamba muda ukifika itajengwa kwa kasi inayotakiwa.
Aidha amekiri Mkoa wa Songwe kuwa na barabara nyingi ni mbovu akisema inatokana na uchanga wake, lakini amesisitza kwamba serikali ya Rais Samia imeanza kazi na ndiyo maana itaanza kujenga barabara ya kwenda Kamsamba kwa awamu.
Leave a comment