DAKTARI Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango nchini Tanzania, ameshindwa kutoa malelezo kuhusu namna ya kulitoa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) shimoni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamejiri wakati Dk. Mwingulu kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Fedha ya 2021/22 leo Jumatano, tarehe 23 Juni 2021 jijini Dodoma.
Mussa Azzan Zungu, Mwenyekiti wa Bunge alihoji, kwanini mpango wa kuboresha utendaji wa ATCL haujaingizwa kwenye muswada huo?
Zungu alihoji baada ya kubaini mabadiliko ya sheria ya kuliboresha shirika hilo, hayamo katika muswada huo uliobeba mapendekezo ya marekebisho ya sheria 22.
Akijibu swali hilo, Dk. Mwigulu amesema, serikali italifanyia kazi suala hilo.
“Mwenyekiti nilipokea hilo suala, sababu mjadala unaendelea ili tuweze kushirikiana Serikali pamoja na kamati, tutakapokuwa tunajibu hoja tutalizungumzia hilo suala,” amesema Dk. Mwigulu.
Hata hivyo, Zungu amesema, kitendo hicho kinakwenda kinyume na kauli iliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan, wakati akihutubia mhimili huo tarehe 22 Aprili 2021, alipoagiza iwekwe mikakati ya kuboresha utendaji wa ATCL.
“Waziri Mwigulu, alipokuja Rais Samia kuhutubia Bunge alizungumzia namna ya kuilea ATCL na kuondoa tozo ambazo ATCL zinalipa, sasa humu hamna,” amesema Zungu.
Zungu amesema, alitarajia kuona serikali inapeleka bungeni mapendekezo ya sheria ya kuiondolea kodi ATCL, ikiwemo ushuru wa ndani na ada ya ndege kutua.
“Maana yake waziri, national carrier (wabebaji wa kitaifa) zote duniani hazilipi local taxes (ushuru wa ndani), landing fees (ada ya kutua). Zote wanalipa ATCL na wanapata matatizo,” amesema Zungu.
Akihutubia Bunge mara ya kwanza baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania, tarehe 19 Machi 2021, Samia alisema Serikali yake itaangalia namna ya kulilea shirika hilo kimkakati, ili liweze kujiendesha kwa ufanisi.
Leave a comment