MKUTANO wa kumi na tano wa bunge unaoanza kesho unatarajia kujadili na kupitisha miswada miwili ya sheria ambayo itasomwa kwa hatua zake zote. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Miswada hiyo ambayo itasomwa ni Mswada wa sheria ya fedha za matumizi kwa mwaka wa fedha 2019 na mswada mwingine ni mswada wa sheria ya fedha wa mwaka 2019.
Kwa mujibu wa ofisi ya kitengo cha mawasiliano na uhusiano wa kimataifa ofisi ya bunge kimeeleza kuwa mkutano unatarajiwa kuanza leo Jumanne saa tatu asubuhi na kumalizika 28 Juni mwaka huu.
Kinaeleza kuwa mkutano huo utakuwa mahsusi kwa ajili ya kujadili utekelezaji wa bajeti za Wizara kwa mwaka wa fedha 2018/19 pamoja na makadirio ya mapato na matumizi ya serikali kwa mwaka wa fedha 2019/20.
Aidha katka mkutano huo kutakuwepo na wastani wa maswali 515 ya kawaida ambayo yataulizwa na kujibiwa na serikali bungeni sambamba na hilo maswali 88 ya papo kwa papo yataulizwa kwa waziri mkuu kila siku ya Alhamisi.
Katika mkutano huo pia kutakuwepo kazi ya kujadili hotuba ya hali ya uchumi wa taifa na bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2019/20 itakayowasilishwa na Waziri wa Fedha na Mipango.
Pamoja na mambo mengine baadhi ya wabunge bila kujali itikadi za vyama vyao wamejipanga kuhoji matumizi halisi ya Sh. 1.5 trilioni ambazo zilionekana kuleta utata kutokana na matumizi yake kutokuwa wazi.
Baadhi ya wabunge ambao wamezungumza na chombo hiki cha habari walisema kuwa katika kuelekea katika uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu ndio mwanya pekee wa kila mmoja kurusha karata zake ili kuona ni namna gani ataweza kurejea mjengoni.
Leave a comment