WAZIRI wa Madini, Doto Biteko, amesema biashara ya madini nchini imeendelea kuimarika huku bei ya madini muhimu kama dhahabu na almasi ikizidi kuongezeka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Biteko ameyasema hayo bungeni leo Ijumaa tarehe 29, Aprili, 2022 wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi yam waka 2022/2023.
Waziri huyo amesema katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi 2022 zimezalishwa jumla ya kilogramu 39,682.94 za dhahabu, kilogramu 7,102.96 za fedha, karati 155,117.10 za almasi.
Pia zimezalishwa kilogramu 15,377.44 za Tanzanite ghafi, kilogramu 130,582.28 za Tanzanite za ubora wa chini (beads), karati 81,305.42 za tanzanite iliyokatwa na kusanifiwa, tani 19,355.13 za madini ya shaba na tani 322.4 za madini ya bati.
Mbali na madini hayo Biteko amesema pia zimezalishwa, kilogramu 6,835,746.73 na karati 12,863.29 za madini mengine ya vito ghafi na vito vilivyokatwa na kusanifiwa mtawalia, tani 18,462,591.96 za madini ya ujenzi.
Aidha zimezalishwa tani 956,688.08 za makaa ya mawe, tani 7,843,634.41 za madini mengine ya viwandani, na tani 51,132.33 za madini mengine ya metali zilizalishwa na kuuzwa.
Kutokana na uzalishaji huo Biteko amesema katika kipindi hicho shilingi 429 bilioni zilikusanywa kama malipo ya mrabaha na ada ya ukaguzi kutoka kwenye madini hayo yenye thamani ya shilingi 6.4 trilioni.
Amesema makusanyo hayo ni ongezeko la asilimia 2.5 ikilinganishwa na shilingi 418.7 bilioni zilizokusanywa katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2020/2021.
Leave a comment