KADA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Hussein Bashe anaweza kuondoka kwenye chama hicho pale kitakapoboronga. Anaandika Faki Sosi … (endelea).
Amesema kuwa, anaweza kufanya hivyo kama alivyofanya Edward Lowassa, Maalim Seif Sharif Hamad na hata Augustino Mrema.
Bashe ambaye ni Mbunge wa Nzega Mjini amesema hayo kwenye mkutano wa kampeni katika Jimbo la Ukonga wakati wa kumnadi mgombea wa chama hicho, Mwita Waitara leo Septemba 12, 2018.
Amesema kuwa, kuhama chama sio dhambi na kwamba alichokifanya Waitara ni haki yake kama walivyofanya wengine wakitoka CCM.
Mbunge huyo kijana anapishana mtazamo na wale wanaosema kuwa, Waitara alinunuliwana na CCM na kwamba, hoja hiyo ni dhaifu.
“Waitara namfahamu toka alipojuwa Umoja wa Vijana wa CCM-UVCCM” amesema Bashe na kuongeza:
“Aliondoka Mzee Augustine Mrema mwaka 1995, Maalim Seif naye akaondola hadi mzee wangu Lowassa alifanya hivyo, hatujawahi kutuhumu kama mtu amenunuliwa.
“Yoyote anapoamua kuwatumikia wananchi anapanda basi, vyama vya siasa ni sawa na basi, ukiona basi hilo dereva, kondakta hamuelewani unaweza kushuka kwenye basi hilo.”
Wakazi wa Jimbo la Ukonga wanatarajiwa kumchagua mbunge wao baada ya Waitara kujivua ubunge na kujiunga CCM ambayo imempitisha kugombea kwenye uchaguzi huo mdogo utaofanyika Jumapili ya Septemba 16 mwaka huu.
Jimbo lingine linalotarajiwa kufanyika uchaguzi siku hiyo ni Monduli pamoja na kata 22 nchini.
Leave a comment