Loy Thomas Sabaya ambaye ni Baba wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya ameshinda nafasi ya Uenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Ushindi huo umekuja baada ya Kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya CCM kilichoketi wiki iliyopita pamoja na mambo mengine, kufanya uteuzi wa mwisho wa wagombea wa nafasi za uongozi ndani ya chama kwa ngazi ya mkoa na wilaya ili kujaza nafasi zilizoachwa wazi kutokana na sababu mbalimbali.
Kupitia uchaguzi huo uliofanyika Ukumbi wa AICC jijini Arusha, Loy Thomas Sabaya ameshinda kwa kupata kura 463 kati ya kura 907 zilizopigwa katika nafasi ya mwenyekiti.
Dk. Daniel Mrisho Pallangyo amepata kura 374, Solomoni Olesendeka Kivuyo amepata kura 59,Edna Israel Kivuyo amepata kura 10 na kura moja ikaharibika.
Uchaguzi huo uliosimamiwa na Mkuu wa Mkoa wa Njombe Anthony Mtaka, umefanyika baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Zelothe Stephen kufariki dunia tarehe 26 Oktoba 2023.
Zelothe alifariki alipokuwa jijini Dar es Salaam, alipokuwa amelazwa kwa matibabu.
Leave a comment