MCHAMBUZI wa masuala ya mifugo, Onesmo Olengurumwa, ameiomba Serikali iwachukulie hatua watu waliochoma vifaranga kutokana na kukosa soko, akisema ni kinyume cha Sheria ya Usalama na Ustawi wa Wanyama ya mwaka 2008. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Olengurumwa ametoa wito huo leo Ijumaa, tarehe 23 Desemba 2022, ikiwa zimepita siku kadhaa tangu shamba la kuku la Kibo, mkoani Kilimanjaro, kuteketeza vifaranga vilivyokosa soko jijini Dar es Salaam.
“Yeyote yule anayefuga wanyama anapaswa kuzingatia haki za wanyama ambazo hazitofautiani na haki za binadamu, mfano kitendo hiki cha kuchoma vifaranga ni kinyume na haki za wanyama na uhuru dhidi ya ukatili na maumivu makali. Sheria hii imekataza mazingira yoyote yanayotweza utu wa mnyama na kumwekea maumivu makali,” amesema Olengurumwa.
Olengurumwa amesema, vifaranga hivyo vilipaswa kutolewa bure kwa wafugaji kama vilikuwa havina magonjwa ya mlipuko.
“Baraza la ustawi wa wanyama au wakaguzi wa wanyama wa eneo hilo wawaite wajieleze ili pia iwe elimu kwa watanzania wengine wanaofuga. Sheria pia inataka kila wilaya kuwe na mkaguzi na mlinzi wa usalama wa wanyama, kama mpo teteeni wanyama,” amesema Olengurumwa.
Leave a comment