ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Moravian la Uamsho Tanzania na Afrika Mashariki, Emmaus Mwamakula, amewataka wagombea Urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020, kutokuwa na roho ya kisasi dhidi ya wapinzani wao mara watakapofanikiwa kushinda kinyang’anyiro hicho. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Askofu Mwamakula ametoa wito huo katika uzinduzi wa Kampeni za Urais za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), zinazofanyika leo Ijumaa tarehe 28 Agosti 2020 katika Viwanja vya Zakhiem Mbagala Dar es Salaam.
Tundu Lissu, Mgombea Urais wa Chadema na mgombea mwenza wake, Salum Mwalimu ndiyo waliopewa dhamana ya chama hicho kugombea.
“Nyie mnaotaka urais, Mungu akiwapa msije kulipa kisasi na kama mkiweka moyoni kisasi anaweza kuwanyanganya,” amesema Askofu Mwamakula.
Askofu Mwamakula amewataka wagombea endapo mmoja wao atafanikiwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Tanzania kutangaza msamaha kwa mahasimu wao waliowaumiza.
Amesema kama wagombea hao wakihifadhi chuki moyoni mwao Mungu hatawapa Urais.
“Mnachotakiwa kufanya ni kutangaza msahama kwa waliokuumiza lakini ukiweka kiburi, mambo ya chuki Mungu hatakupa na wote mkisema uko tayari kuwapenda kuwakumbatia, hakika Mungu atakupa utawala na atakupa kibali,” amesema Askofu Mwamakula.
Kiongozi huyo wa kiroho amemtaka, Tundu Lissu na mgombea wake mwenza, Salum Mwalimu, kama Mungu atawapa kibali cha kushinda kuwatetea Watanzania wanyonge.
“Ninyi mnaogombea, endapo Mungu atawapa kibali kuongoza nchi jambo la muhimu ni kutenda haki, mkitenda haki Mungu ndio atakayetoa amani.”
“Sababu Mungu ndiye analinda amani, watu wakitenda haki na huiondoa amani watu wasipotenda haki na kunapokuwa hakuna haki haileti amani hadi watu watende haki,” amesema Askofu Mwamakula.
Naye Sheikh Rajab Katimba kutoka Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha kampeni hizo zinafanyika kwa amani sambamba na kuhakikisha vinatoa haki kwa vyama vyote.
“Tunazindua kampeni rasmi leo ambazo tunategemea zitakuwa ‘fair play’ kwa chama husika bila kujali ukubwa wala udogo wa chama. Tunategemea vyombo vya utoaji haki na usalama vitatoa haki endapo havitatoa haki Mungu anza kuviadhibu hapa hapa duniani na huko akhera.”
“Tunataraji utulivu utatamalaki lakini hayo yatawezekana kama kutakuwa na haki kwa maana haki ni tunda la amani,” amesema Sheikh Katimba.
Leave a comment