ASKOFU wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Karagwe Mkoa wa Kagera, Dk. Benson Bagonza ametoji maswali nane juu ya tozo za miamala ya simu na majengo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kagera … (endelea).
Tangu kuanza kwa tozo hizo, zimeibua mjadala kwa wananchi huku Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan ikiahidi kupitia malalamiko yao.
Kupitia ukurasa wake wa kijamii wa Facebook, Askofu Bagonza ameandika maswali nane akihoji juu ya tozo hizo na ugumu wa maisha ambayo wananchi wanapitia.
Maswali hayo ni;
1. Wasamaria wema wamemuokota aliyegongwa na gari barabarani. Wakamkimbiza hospitali. Daktari anataka laki tatu kumtibu. Linaundwa group kuchangisha. Serikali inakata tozo badala ya kulipia matibabu ya raia wake!
2. Wawili wamependana. Wanatualika tule pilau ili waoane vizuri. Tunachangishana ili kuwapunguzia makali. Serikali inakata tozo badala ya kuwachangia ili waoane vizuri.
3. Mjaluo kafia Dar alikoenda kutoa mahari ya mke wa saba. Sharti aziikwe Taarime. Tunachangishana kusafirisha. Serikali inakata tozo badala ya kuchangia ubani ili tulio msibani tule Kamongo.
4. Wakurya wamejifunza kutumia choo. Wameamua kujenga choo shuleni kwao. Wakatuma michango kupitia what’s up. TOZO ya serikali iliyokatwanni sawa na tundu moja la choo. Hivi Serikali haijawazuia Wakurya kutumia choo ili waendelee kujisaidia vichakani?
5. Shule ya kata inalipia umeme kwa Luku, makanisa, misikiti, mortuary, vyoo vya umma,nk vinalipia umeme kupitia LUKU. Majengo haya yamesamehewa kulipa kodi ya majengo. Je kulipia kodi hii kupitia LUKU hakufuti misamaha hiyo?
6. Wazee wenye miaka 60 na zaidi walisamehewa kulipa kodi ya majengo. Kwa kutumia Luku kulipa kodi hii, msamaha wao umefutwa. Wanarejea kuwa vijana! Waliokuwa waajiriwa warudi kazini?!
7. Viwango vya tozo na kodi ya pango ni vikubwa. Miundombinu ya kampuni za simu imegharimu fedha nyingi sana na tayari wanalipa kodi na kutoa ajira. Watumiaji wa umeme vijijini wengi ni Maskini Sana wanaoishi kwa huruma ya TASAF isiyo rasmi. Wanahitaji kunyweshwa maziwa badala ya kukamuliwa.
8. Tumeulizwa tuna mapendekezo gani ya kuzipa pengo la bajeti endapo tozo zitafutwa? Kama mko tayari kusikiliza tutapendekeza. Wengi tunatamani serikali inayosikiliza kuliko inayodai kusikilizwa.
Tozo ni mbaya na ni kubwa. Kodi ya pango kupitia LUKU ni kero na inazua maswali mengi. RUDINI mezani, punguza kusema, ongeza kusikiliza. Sikiliza wanaokosoa kuliko wanaopongeza.
Kifo cha mbwa huanza kwa kupoteza uwezo wa kunusa.
Asante askofu kwa kusema ukweli kuhusu kero hizi kubwa nchini. Hongera
Ukweli ni kuwa serikali imeshindwa kukusanya kodi kwa njia za kawaida na sasa imetafuta njia rahisi na za mkato kwa kuwabana na kuwakamua wananchi hata wasiohusika
Tuanze na madini yetu. Tunaambiwa TZ tumebarikiwa kuwa na madini mengi na mbalimbali. Lakini tunafanya Vibaya kuendelea kuamini watu wa nje na kukosa mapato ya kutosha.
Kuendelea kukamua watu badala ya madini ni utumwa mamboleo.
Asante kwa kuiweka taarifa ya aina hii humu.
Pengine italeta chachu ya aina yake.
Rafiki yenu,
Aliko Musa.
Mbobezi Kwenye Majengo.