ASKOFU wa Kanisa la Mlima wa Moto, Jimbo la Dodoma na Nyanda za Juu Kusini, Sylvanus Komba amewataka vijana kuacha kukaa vijiweni na badala watafute kazi za kufanya. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Ametoa wito huo leo tarehe 16 Agusti 2020 wakati akihubiri katika ibada ya Jumapili iliyofanyika kwenye kanisahilo lililopo Sabasaba jijini humo.
Askofu Komba akihubiri juu ya ibada maalumu ya maombezi yaliyolenga kuwakomboa watu waliofungwa na kuwaondolea yanayowazuilia baraka zinazotakiwa kutokea kwao, amesema ni wakati sasa wa kila mmoja kufanya kazi kwa bidii ili aweze kuvuna alichopanda.
Amesema, maandiko yanaeleza wazi kuwa kila mmoja anatakiwa kufanya kazi ili aweze kuvuna alichokipanda na kwamba, asiyefanya hivyo tayari ataishi kwa kulalamika na kuwa masikini.
Akiwahubiria waumini wake amesema, wakati wa kusubiri misaada mbalimbali umeisha na kinachotakiwa ni kila mmoja kufanya kazi.
“Nataka niwaambie waumini wangu umefika wakati wa kila mmoja kufanya kazi kwa mikono yake, na kufanya kazi ni maelekezo sahihi kutoka katika maandiko matakatifu.
“Maandiko yanasema, wakati wa kula chakula cha neema ni mwaka mmoja hadi miwili, lakini mwaka wa tatu ni mwaka wa kuchukua mbegu na kupanda na mwaka unaofuata ni mwaka wa kuvuna,” amesema Askofu Komba.
Kuhusu utumiaji wa mitandao ya kijamii, Askofu Komba amekemea wale ambao wanatumia mitandao hiyo kutukana watu wengine au kuwachafuana.
“Wapo baadhi ya watu ambao wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kwa lengo la kuwachafua watu wengine au kutengeneza chuki kati ya mtu na mtu.
“Mitandao hiyo ya kijamii yafaa kutumiwa kwa masilahi mapana ya mtu mmoja mmoja au kikundi kwa ajili ya maendeleo, sio kusababisha chuki, ugomvi au mambo ambayo hayastahili,” amesema.
Leave a comment