IMEELEZWA kuwa asilimia 30 ya watoto wenye umri kuanzia siku 0 hadi miaka nane wanakabiliwa na udumavu wa akili huku mikoa yenye uzalishaji mkubwa wa chakula inaongoza kwa kuwa na watoto enye changamoto hiyo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma (endelea).
Hayo yamebainishwa hivi karibuni na Naibu Katibu Mkuu ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dk. Wilson Mahera wakati wa kufunga mafunzo ya Kitaifa ya sayansi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto yaliyofanyika jijini Dodoma kwa muda wa siku sita.
Dk. Mahela alisema kutokana na takwimu hizo, Serikali imeona umuhimu wa kupambana na hali hiyo ili kupata watoto ambao watakuwa na utimilifu wa akili.
Alisema hali hiyo litasidia kuwa na Taifa lenye watu wanaoweza kuzalisha na kuwa viongozi bora.
Alisisitiza kuwa kwa sasa Serikali inatoa elimu kuanzia ngazi ya chini ya maofisa ustawi wa jamii hadi kwa ngazi ya Taifa kwa nia ya kila mzazi kutambua umuhimu wa lishe kwa mtoto, haki, ulinzi na kukuza uelewa kuwa mtoto.
Alisema mtoto akifanyiwa mambo hayo atakuwa amejengewa uwezo mkubwa wa kumuondolea janga la udumavu wa akili.
Aidha, alisema licha ya kuhakikisha watoto wa umri huo wanapatiwa lishe bora pia watoto wanatakiwa kulindwa na kupewa uhuru wa kujieleza na siyo kuwafanya kuwa watu wa kuelezewa tu.
“Takwimu za sensa iliyipita inaonesha wazi kuwa jumla ya watoto wenye umri wa kuanzia siku 0 hadi miaka nane ni milioni 16 ambao kimsingi ni wengi.
“Kama watakuwa wamepata malezi mazuri na kuwakinga na udumavu wa akili, ni wazi kuwa taifa litakuwa na watumishi hodari na bora, wachumi wazuri, madaktari wenye ueledi mpana pamoja na kuwa na Taifa lenye wazalishaji wakubwa zaidi” amlieleza Dk. Mahera.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya kitaifa ya sayansi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto akiwemo Afisa ustawi wa jamii Mkoa wa Manyara, Khadija Muwango na Musa Masongo wa Shirika la TAHEA Mwanza, walisema ili mtoto akue vizuri kimwili na kiakili, anahitaji chakula bora au mlo kamili.
“Mlo kamili unajumuisha vyakula vyenye virutubisho kama protini, wanga, mafuta, vitamini na madini,” alisema.
Leave a comment