TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Manyara, inamshikilia mkazi wa Mjini Babati, Yuda Sendeu akidaiwa kuzuia Sh. 44.7 milioni fedha za chama cha kuweka na kukopa cha Babati Saccos. Anaripoti Mwandishi Wetu, Manyara … (endelea).
Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Manyara, Holle Joseph Makungu akizungumza mjini Babati leo Jumamosi tarehe 8 Agosti 2020 amesema, Sendeu alichukua mkopo wa Sh.35 milioni na kutakiwa kurejesha Sh.44.7 milioni.
Makungu amesema, Sendeu alichukua mkopo huo mwaka 2010 na alitakiwa kurudisha mkopo huo baada ya miezi 24 pamoja na riba.
Amesema uchunguzi unaonyesha Sendeu alifanya makubaliano ya kihalifu na baadhi ya wanachama wa Babati Saccos waliochukua fedha katika Saccos hiyo bila kurejesha.
Amesema walifanya hivyo ili haki za wanachama waaminifu wa Saccos hiyo ziweze kupotea.
“Hadi wanachama waaminifu wa Saccos hiyo wanafikisha malalamiko ya dhuluma hiyo Takukuru, Sendeu bila kustahili amekaa na fedha hizo kwa miaka 10,” amesema Makungu.
Ametoa rai kwa wanachama wa Babati Saccos wanaofahamu kuwa wamechukua fedha za Saccos hiyo na muda wa kurejesha umepita wafike kwa hiyari kwenye ofisi za Takukuru.
Amesema wanatakiwa wafike kwenye ofisi hizo tarehe 10 Agosti 2020 ili wapewe hesabu zao na kuzirejesha na kwa wale watakaokaidi hatua kali dhidi yao zitachukuliwa kuanzia 12 Agosti 12 2020.
Leave a comment