Shirika la Amend Tanzania kwa kushirikiana na Ubalozi wa Uswisi linatarajiwa tena kuanza kutoa mafunzo ya elimu ya usalama barabara ni kwa madereva wa bodaboda katika kata mbalimbali za jiji la Dodoma ili kuunga mkono jitihada za serikali kudhibiti janga la ajali nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Awamu ya pili ya mafunzo hayo imekuja baada ya Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri kuomba mafunzo hayo yatolewe tena kwa kata zilizosalia.
Katika mafunzo ya awali ambayo yalitolewa Februari mwaka huu, jumla ya madereva bodaboda 250 waliopatiwa mafunzo hayo.
Msaidizi wa Miradi kutoka Shirika la Amend, Amiri Matimba amewaambia waandishi wa habari kwamba mafunzo hayo yataanza kutolewa leo tarehe 15 Aprili 2024 katika kata ambazo hazikupata mafunzo hayo yalipotolewa Februari mwaka huu.
Amefafanua mafunzo hayo yananalenga kuboresha usalama wa waendesha pikipiki, abiria na watumiaji wengine wa barabara, hivyo kuzuia vifo na majeruhi wa matukio ya ajali ambapo wengi wao ni vijana.
Ameongeza kuwa Amend na Ubalozi wa Uswisi wamekubali ombi la mkuu wa wilaya ya Dodoma na kwamba mafunzo yanaanza rasmi leo Jumatatu na wadau mbalimbali watashiriki likiwemo Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama barabarani Wilaya ya Dodoma.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Walimu wa Usalama Barabarani, Mwalimu Massava Ponera amewataka maofisa usafirishaji (bodaboda)kujitokeza kwa wingi kupata elimu hiyo ambayo ni muhimu kwa shughuli zao.
“Mafunzo ya elimu ya usalama barabarani yana umuhimu makubwa kwani mbali na vifo ajali za barabarani husababisha ulemavu wa kudumu huku takwimu za sensa nchini zikionesha kuwa asilimia kubwa ya Watanzania ni vijana na wengi wameamua kujikita katika ujasiriamali wa bodaboda.”
Leave a comment