CHAMA cha siasa cha upinzania nchini Tanzania cha ACT-Wazalendo kimetangaza kutoshiriki kikao baina ya jeshi la polisi na ofisi ya msajili wa vyama vya siasa nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kikao hicho kimepangwa kufanyika tarehe 21 Oktoba 2021 jijini Dodoma, kikihusisha wadau wa siasa na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro.
Lengo la kikao hicho ni kutafuta njia bora ya kuendesha shughuli za kisiasa.
Leo Jumapili, tarehe 26 Septemba 2021, ACT-Wazalendo imetoa taarifa iliyosainiwa na Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma, Salim Bimani ikisema, baada ya tafakuri ya kina, wamekubaliana kutoshiriki kikao hicho huku wakitoa hoja tatu.
ACT-Wazalendo inaungana na chama kikuu cha upinzania nchini humo cha Chadema kususia kikao hicho. Chadema kilikwisha sema, hakioni sababu ya kushiriki kikao hicho kwani Katiba na sharia zinawaruhusu kufanya shughuli za kisiasa hivyo mamlaka husika zizifuate.
Mosi; tarehe 21 hadi 22 Oktoba 2021, viongozi wakuu wa ACT Wazalendo watakuwa kwenye mkutano mkuu wa kitaifa wa haki, amani na maridhiano ulioitishwa na Kituo Cha Demokrasia Tanzania (TCD).
Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na Rais Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Pili; baada ya msajili wa vyama vya siasa, Jaji Francis Mutungi kutangaza kikao cha polisi na vyama vya siasa, ACT Wazalendo kupitia Kiongozi wa chama, Zitto Kabwe walimwandikia msajili kuwa kikao hicho kimjumuishe Waziri wa Mambo ya Ndani ambaye ndiye mwenye dhamana ya kisiasa ya Jeshi la Polisi.
“Hadi sasa hatujapata mrejesho wa suala hilo na mwelekeo ni kuwa kikao hicho kitakuwa cha Polisi na vyama vya siasa pekee,” amesema Bimani.
Tatu; Bimani amesema “matamshi ya IGP Simon Sirro baada ya kikao chake na msajili wa vyama vya siasa hayaoneshi nia njema ya kikao hicho.”
“Kauli yake kuwa nchini Tanzania hakuna shida kuhusu mikutano ya nje na kwamba tatizo lipo kwenye mikutano ya ndani na inabidi sheria iwekwe sawa ni dalili ya wazi kuwa kikao hicho kinaweza kutumika kubinya zaidi shughuli za kisiasa nchini,” amesema
Leave a comment