MOHAMMED Said Issa, ameteuliwa na Chama cha ACT-Wazalendo, kugombea Jimbo la Konde, visiwani Zanzibar, katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika tarehe 18 Julai 2021. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 24 Juni 2021 na Katibu wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma, Salim Bimani.
Kwa mujibu wa taarifa ya Bimani, Issa amepitishwa kugombea nafasi hiyo na Kamati Maalumu ya ACT-Wazalendo.
“Leo kamati maalumu ya chama kwa upande wa Zanzibar, imekutana katika kikao cha dharura kwa ajili ya uteuzi wa mgombea ubunge Jimbo la Konde, Mkoa wa Kaskazini Pemba, utakaofanyika tarehe 18 Julai 2021, kwa kauli moha imemteua Issa kuwa mgombea ” imesema taarifa ya Bimani.
Taarifa hiyo imesema, kamati hiyo ilimpitisha Issa kugombea jimbo hilo, baada ya kupokea taarifa ya uchaguzi wa kura za maoni za kumpata mgombea, katika uchaguzi huo mdogo, zilizofanyika tarehe 23 Juni 2021.
Uchaguzi huo mdogo katika Jimbo la Konde, uliitishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), baada ya aliyekuwa mbunge wake kupitia ACT-Wazalendo, Khatib Said Haji, kufariki dunia tarehe 20 Mei 2021, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu.
Mwili wa Khatibu ulizikwa siku hiyo hiyo, nyumbani kwao Pemba visiwani Zanzibar.
Leave a comment