CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimemtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kufanya ukaguzi dhidi ya fedha za tozo za miamala ya simu pamoja na za mkopo wa kukabiliana na athari za Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19), kiasi Cha Sh. 1.3 trilioni, ili kubaini matumizi yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 17 Juni 2023, jijini Dar es Salaam na Waziri Kivuli wa Fedha na Uchumi wa ACT-Wazalendo, Ester Thomas, wakati akichambua bajeti pendekezwa ya Serikali Kwa mwaka wa fedha wa 2023/24.
Ester amedai kuwa, wa sasa kuna mkanganyiko juu ya matumizi ya fedha hizo katika utekelezaji wa miradi, hivyo CAG anapaswa kuzikagua ili kubaini ukweli wake.
Amedai Serikali inasema inatekeleza miradi muhimu ya huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu na maji kwa kutumia fedha hizo kwa wakati mmoja.
“Tunashauri CAG kufanya ukaguzi maalum wa matumizi ya fedha zote zinazopatikana kwenye tozo na ukaguzi huu ni muhimu sana kwani Kuna mkanganyiko kuhusu matumizi ya fedha za tozo na fedha zilizopatikana za UVIKO-19,” amedai Ester.
Ester amedai “tuliambiwa zitaenda kuleta huduma za kijamii na kuboresha hali ya maisha kwa Watanzania kwa kuleta elimu, afya na maji. Lakini bado tuna maswali mengi kuhusu tozo yetu inakwenda wapi.”
Fedha za tozo ya miamala ya simu zilianza kutozwa na Serikali Julai 2021, ambapo ilisema zinakwenda kuboresha miundombinu ya maji, barabara na elimu.
Pia, mnamo 2021 Serikali ilipokea mkopo wa fedha za UVIKO-19 kiasi cha Sh. 1.3 trilioni, kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF), kwa ajili ya kukabiliana na athari za janga hilo.
Ambapo Serikali ilisema inazitumia fedha hizo kuboresha huduma muhimu za jamii, hususan maji, afya na elimu.
Leave a comment