Waziri Mkuu Kasim Majaliwa amesema fedha nyingi za mapato yanayokusanywa katika halmashauri kongwe ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe zinaishia katika mifuko ya watu binafsi ambao majina yao anayo.
Amesema inashangaza halmashauri ya Mbozi inakusanya Sh bilioni nne ilihali Tunduma ambayo ni halmashauri change ikikusanya Sh bilioni 13. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Kupitia mkutano wa hadhara uliofanyika leo Jumamosi katika stendi ya Malori mkoani hapa, Majaliwa amesema mbali na kukusanya mapato kidogo pia viongozi wa halmashauri hiyo hawana ubunifu wa kubuni vyanzo vipya vya mapato.
Amesema hata hiyo Sh bilioni nne wanayokusanya haionekani inafanya kazi gani kwani miradi yote inajengwa kwa fedha za serikali kuu.
“Mapato ya Sh bilioni nne mnayokusanya kwa mwaka ni kiduchu ukilinganisha na ukongwe wa wilaya, fedha nyingi zinaingia mifukoni mwa watu, majina yote ya wezi ninayo,” amesema.
Awali, mbunge wa Vwawa, Japhet Hasunga (CCM) alimuomba waziri mkuu kuipandisha hadhi halmashauri ya Mbozi kuwa manispaa.
Pia amemuomba kutatua changamoto ya ukosefu wa stendi kuu na soko la pamoja la kuuzia mazao.
Akijibu maombi hayo, Majaliwa amesema suala la kupanda hadhi kuwa manispaa sio shida bali tatizo ni vigezo ikiwamo makusanyo ya fedha na mpangilio wa majengo.
“Makusanyo ya Sh bilioni 4 mnazokusanya kwa mwaka ni madogo ukilinganisha na ukongwe wa halmashauri yenu. Tunduma ni wachanga lakini wanakusanya Sh bilioni 13. watumishi, madiwani hamna ubunifu,” amesema Majaliwa.
Amesema Mbozi ni halmashauri kongwe nchini na ina vyanzo vingi vya mapato, ikiwemo makusanyo makubwa yatokanayo na zao la kahawa lakini makusanyo yake ni madogo huku mji huo ukiwa umezorota.
Amesema Tunduma imezidiwa na uwingi wa malori hivyo halmashauri hiyo inatakiwa kutenga eneo pembezoni mwa barabara na kuweka uzio kwa ajili ya kulaza magari yatakayotozwa fedha na kuingiza kipato.
Leave a comment