RAIS Samia Suluhu Hassan amevitaka vyama vya siasa kutohodhi mchakato wa marekebisho ya katiba, akisema suala hilo si mali yao bali ni mali ya wananchi wote. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akifungua mkutano maalum wa Baraza la Vyama vya Siasa, leo tarehe 11 Septemba 2023, jijini Dar es Salaam, Rais Samia amewataka wanasiasa kutowaburuza wananchi kuhusu mabadiliko ya katiba.
Mkuu huyo wa nchi, amesema mchakato huo utaanza na utoaji elimu kwa wananchi ili waielewe katiba, kwa kuwa asilimia kubwa hasa walioko vijijini hawaijui vyema.
“Tunaanza na elimu ya katiba, watanzania wajue ni kitu gani, wajue kinasemaje na kina nini sababu tunakokwenda viongozi wa kisiasa tunadhani tuna haki ya kuburuza watu.
Tunachokisema sisi watu wote wafanye hivyo. Katiba si kitabu ni morality ethical standard, tutaenda kwa mwendo huu kila mtu ajue,”amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema “tuna kazi kubwa ya kuwafanya watanzania waijue katiba ni nini na hiko kitabu kimekaaje. Wengine hawakijui ukienda huko vijijini mtu anaweza akaja na Ilani ya CCM akakwambia katiba, hajui ilani inasemaje wala katiba inasemaje hawajui.”
Katika hatua nyingine, Rais Samia amesema kamati maalumu itaanzishwa kwa ajili ya kusimamia mchakato huo, ambapo vyama vya siasa vitatoa uwakilishi wake.
“Tusiwaburuze, katiba viongozi wa siasa si yetu ni mali ya watanzania. Mwisho wa mkutano huu nimemwambia msajili nataka viongozi wa vyama walete maoni yao kwenye kamati itakayokwenda kuanzisha mchakato wa katiba na ninyi mtakuwa na wawakilishi wenu sio kila mtu ataingia kule,” amesema Rais Samia.
Msimamo wa Rais Samia kuanza kutoa elimu kwa wananchi juu ya katiba, umepinga vikali na baadhi ya makundi ikiwemo asasi za kiraia, ambayo yameshauri mchakato huo uanze moja kwa moja katika marekebisho kwa madai kuwa elimu ilishatolewa hapo awali.
Leave a comment