RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewatunuku kamisheni maafisa wanafunzi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) 724 waliohitimu mafunzo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Amiri Jeshi Mkuu huyo wa nchi, ametunuku kamisheni hizo leo Jumamosi, tarehe 26 Novemba 2022, katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli, jijini Arusha.
Akizungumza baada ya kuwatunuku kamisheni hizo, Rais Samia amekipongeza chuo hicho pamoja na Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), kwa kuendelea kushirikiana katika kutoa mafunzo kwa maafisa wa jeshi yenye lengo la kuwa na ubora wa hali ya juu.
“Nawapongeza kwa kuendelea na ushirikiano wa kutoa mafunzo ya pamoja kuhakikisha wanajeshi wetu wanakuwa na ubora wa hali ya juu. Ushirikiano huu ni mzuri kwa jeshi letu na taifakwa ujumla. Nawapongeza wahitimu wote wa mafunzo ya shahada ya sayansi ya kijeshi,” amesema Rais Samia.
Kati ya maafisa waliotunukiwa kamisheni hizo, wanaume ni 635 na wanawake 89, ambao wana elimu katika madaraja tofauti ikiwemo kidato cha sita, stashahada, stashahada ya juu na stashahada ya kwanza.
Miongoni mwao, wanafunzi 109 walitunukiwa kamisheni na Rais Samia, baada ya kuhitimu shahada ya sayansi ya kijeshi, waliyoanza kusoma Novemba 2019. Awali walikuwa 119 lakini 10 waliachishwa mafunzo kwa sababu mbalimbali ikiwemo za kiafya, nidhamu na kutoroka mafunzo.
Maafisa wengine waliotunukiwa kamisheni ni 20, waliopata mafunzo nje ya Tanzania katika nchi za China, India, Kenya, Misri na Urusi.
Leave a comment