MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Heche, amewataka wananchi wajikite katika kuibadilisha nchi akidai mabadiliko na maendeleo hayataletwa na viongozi kwa kuwa wameridhika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Lindi…(endelea).
Heche ametoa kauli hiyo jana Ijumaa, tarehe 26 Novemba 2022, akizungumza katika kongamano la kudai katiba mpya, liliofanyika kwenye Jimbo la Mtama mkoani Lindi.
“Nani mnasubiri awabadilishie nchi yenu? Hamuwezi kutegemea mtu sababu binadamu anabadilika, tulikuwa na Halima Mdee tulimuamini ametubadilikia. Malengo yetu ndiyo yanayotuunganisha sio mtu. Mabadiliko duniani hayaletwi na watalawa sababu watawala wako kwenye hali ya kuridhika, mabadiliko yataletwa na vijana na masikini sababu hawana cha kupoteza cha kupoteza kwao ni umasikini na mabadiliko ni kwa ajili ya hali nzuri ya kwao,” alisema Heche.
Mbunge huyo mstaafu wa Jimbo la Tarime Vijijini, alidai Serikali imeshindwa kutimiza ahadi yake ya kupunguza ukali wa gharama za maisha, badala yake gharama hizo zimepanda huku kipato cha mwananchi kikibaki pale pale.
“Ndugu zangu wamekuwa wakiwaahidi watapunguza gharama za maisha, hazipungui zinazidi kuwa mbaya. Chumvi, sukari kila kitu kinapanda na kipato chako kiko palepale. Sasa mimi nimekuja kuwaambia tuamke,” alisema Heche.
Katika hatua nyingine, Heche aliishauri Serikali ipunguze kukopa fedha ili kudhibiti ongezeko la deni la taifa kwa ajili ya kukwepa kutumia fedha nyingi kulilipa badala ya kuzipeleka katika kuwahudumia wananchi.
“Ndani ya mwaka mmoja Serikali imekopa Sh. 8.7 trilioni sawa na asilimia 14 ya deni lote walilokopa viongozi waliopita. Tunakopa kila siku leo hatuna madaktari vijana wamemaliza vyuo hawawezi kuajiriwa kwa sababu Serikali hela inalipa deni la taifa,” alisema Heche.
Leave a comment