WIZARA ya Afya ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imetoa taarifa ya ongezeko la wagonjwa wapya sita (6) wa Corona (COVID-19). Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Kupitia taarifa iliyotolewa leo tarehe 16 Aprili 2020 na Waziri wa Afya visiwani humo, Hamad Rashid inaeleza kuwa idadi hiyo ya wagonjwa inapelekea kufikia idadi ya wagonjwa 24 kutoka 18 ambao waliripotiwa awali ambapo wagonjwa hao watano ni wanaume, mmoja mwanamke na wote ni raia wa Tanzania.
“Wagonjwa wote ni raia wa Tanzania na hawana historia ya kusafiri nje ya nchi siku za hivi karibuni, wote wamelazwa katika vituo maalum kwa ajili ya matibabu,” imeeleza taarifa hiyo.
Wagonjwa hao ni Mwanaume (30) mkazi wa Kibweni, Mwanaume (27) mkazi wa Magogoni, Mwanaume (28) mkazi wa Kwarara, Mwanamke (58) mkazi wa Kilimahewa Juu, Mwanaume (23) mkazi wa Amani na Mwanaume (55) mkazi wa Kidoti.
Aidha, Serikali ya Zanzibar imeendelea kuwasisitiza wananchi kuchukua tahadhari zote za kujikinga na ugonjwa wa Corona na kuwataka wananchi wanaofikwa na misiba mbalimbali kuchukua tahadhari jinsi ya kushughulika na taratibu za mazishi na kuwa wanashauriwa kushirikiana na wataalamu wa afya kwa kupata miongozo sahihi.
Leave a comment