MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Prof. Mussa Assad, amezitaka asasi za kiraia kuhakikisha zinasaidia kulinda rasilimali za asili, ikiwemo madini ambazo zimekuwa zikitumika vibaya. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Prof. Assad ametoa kauli hiyo leo tarehe 1 Julai 2019 jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya madini, mafuta na gesi yanayotolewa kwa wadau 80 kutoka Asasi mbalimbali zisizo za serikali nchini.
Amesema, lengo la mafunzo hayo ni kupata uelewa katika eneo hilo jipya la sekta ya madini, mafuta na gesi ili kusaidia kulinda rasilimali hizo.
“Rasilimali zetu za asili zimekuwa zikitumika vibaya hasa nyakati hizi, hivyo kila mmoja wetu anafahamu ubadhirifu unaoendelea katika nyanja mbalimbali zinazohusu sekta ya madini, mafuta na gesi, mafunzo haya yatatusaidia kuelewa na kuzilinda rasilimali hizi,”amesema
Prof. Assad amesema, mafunzo hayo yamefadhiliwa na Benki ya Dunia (WB) kwa kusaidiana na ofisi yake ili kuhakikisha wadau hao wanapata mafunzo ya kuwajengea uwezo wa uelewa wa sekta hizo.
“Wawezeshaji wetu ni kutoka taasisi ya KPMG ambao ni wataalam kwenye maeneo haya ya madini, mafuta na gesi na wataendesha mafunzo haya kitaalam yatasaidia kuongeza thamani na tija,” amesema.
Amewataka wadau hao kushiriki kikamilifu ili kila mmoja kupata uelewa wa kina, ambao utasaidia kwenye majukumu yao.
Wakizungumza kwenye mafunzo hayo, baadhi ya wadau wamesema, mafunzo hayo ni muhimu yakashushwa ngazi za chini ili Watanzania wawe na uelewa wa kutosha wa kulinda rasilimali hizo.
Akitoa mada kuhusu sekta ya gesi na mafuta, Mbia wa KPMG Tanzania, Alexander Njombe amesema, Tanzania kuna gesi futi za ujazo Trilioni 57.54 ambazo zinaweza kutumika miaka 50 bila kuisha huku kati ya hizo futi za ujazo Trilioni 10 zipo sehemu ya nchi kavu.
Leave a comment