RAIS John Magufuli amefanya mazungumzo na Afisa Mwendeshaji Mkuu wa Kampuni ya Barrick Gold anayeshughulikia Afrika na Mashariki ya Kati, Dk. Willem Jacobs kuhusu utekelezwaji wa makubaliano yaliyofikiwa tarehe 19 Oktoba 2017 kati ya serikali na kampuni hiyo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Miongoni mwa makubaliano yaliyofikiwa na serikali pamoja na Kampuni hiyo mwaka 2017, ni pamoja na Barrick Gold kuipa Tanzania dola za kimarekani 300 milioni kama malipo ya kuonesha nia njema ya kufidia fedha zilizotokana na upotevu wa mapato, na kulipa hisa ya asilimia 16 ya mgawo wa asilimia 50 ya mapato ya mauzo ya dhahabu kutoka katika migodi mitatu inayoimiliki.
Akizungumza katika kikao chake na Rais Magufuli kilichofanyika leo tarehe 20 Februari 2019 Ikulu jijini Dar es Salaam, Dk. Jacobs amesema dhumuni la kikao hicho ni kumhakikishia Rais Magufuli kuwa makubaliano hayo watayatekeleza kikamilifu.
Dk. Jacobs amemhakikishia Rais Magufuli kwamba hakuna kitakachobadilika katika makubaliano yaliyofikiwa awali yaliyoongozwa na Mwenyekiti Mtendaji wa Barrick Gold Corporation, Prof. John Thornton ambapo miongoni mwa makubaliano hayo ni kuilipa Tanzania kifuta machozi cha dola 300 milioni ambayo ni sawa na zaidi ya Sh. 682 bilioni.
Waziri wa katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi amesema nyaraka za makubaliano hayo zimekamilika na kwamba kinachosubiriwa ni utekelezaji wa makubaliano hayo unaotarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Machi mwaka huu.
“Baada ya muungano wao, hii sasa ni timu mpya na tumewaona ni watu ambao sasa wapo tayari kutekeleza yale yote yaliyokubaliwa, na sasa ni kwa kila upande kwenda kwenye vyombo vyake vinavyohusika kufanya maamuzi ya mwisho ili utekelezaji ufanyike,” amesema Prof. Kabudi.
Leave a comment