SERIKALI kupitia Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Harison Mwakyembe ameeleza sababu za ndege ya serikali aina ya Dreamliner kushindwa kuisafirisha timu ya taifa ya Tanzania Taifa Stars nchini Cape Verde, ni baada ya kukosa uwanja wa kutua ndege hiyo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Hapo awali serikali ilitoa ndege hiyo kwa ajili ya kusafirisha kikosi hicho kinachokwenda kupambana na Cape Verde ili kuwania tiketi ya kufuzu kwa Kombe la Mataifa Afrika linalotarajia kufanyika mwakani nchini Cameroon.
Baada ya kukosekana ndege hiyo Waziri Mwakyembe alisema kuwa wameongea na Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) na wamefanikiwa kuagiza ndege nyingine yenye usajili wa Tanzania ambayo itabeba wachezaji pamoja na viongozi wanaotarajia kuondoka leo majira ya saa 5 usiku.
“Kiwanja cha Praia ambao ni mji mkuu wa Cape Verde ni kidogo na njia yake ya ndege ni ndogo ina urefu wa kilomita 2.1 wakati ndege yetu Dreamliner inahitaji kilomita 3 ili iweze kutua,” alisema Mwakyembe.
Mwakyembe aliongezea kuwa wachezaji wamepewa vipaji kwa ajili ya kulipambania taifa na kuleta tabasamu kwa watanzania wengine, taifa lipo nyuma ya timu na tuna hakikisha tunafuzu kwenda Cameroon ndio maana Serikali imehakikisha tunapata ndege binafsi.
Timu hiyo imeagwa mapema leo na kwenda kucheza mchezo wake wa tatu katika kundi L, siku ya Ijumaa 12, Octoba 2018 dhidi ya Cape Verde na siku nne baadae watacheza mchezo wa marudiano kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Leave a comment