WAZIRI wa Fedha na Mipango nchini Tanzania, Dk. Philip Mpango amebainisha changamoto tano ambazo zinaikabili wizara hiyo ikiwamo mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea)
Dk. Mpango amebainisha changamoto hizo leo Ijumaa bungeni jijini Dodoma tarehe 15 Mei, 2020 wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi kwa wizara yake ya mwaka 2020/21.
Amesema, utekelezaji wa majukumu ya wizara yanakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo tunaendelea kukabiliana nazo kwa kushirikiana na wadau wengine ili zisilete athari hasi katika malengo yaliyojiwekea.
Amezitaja baadhi ya changamoto hizo ikiwamo ya corona ni; kasi ndogo ya ufuatiliaji na tathmini ya miradi na programu za maendeleo katika wizara, idara zinazojitegemea, wakala, taasisi za umma, sekretarieti za mikoa na mamlaka za serikali za mitaa.
Nyingine ni; mabadiliko ya mara kwa mara ya teknolojia ya mifumo ya usimamizi na ukusanyaji wa mapato yanayoleta uhitaji wa upatikanaji wa teknolojia mpya na kuboresha na kuhuisha teknolojia ya mifumo iliyopo ili kuongeza ufanisi.
“Kuongezeka kwa gharama za mikopo kwenye masoko ya fedha duniani kutokana na mabadiliko ya sera za fedha katika nchi zilizoendelea (hususan Marekani na Nchi za Ulaya,” amesema Dk. Mpango
Amesema, uharibifu wa miundombinu ya barabara na madaraja kutokana na mafuriko.
Dk. Mpango amebainisha mikakati ya kukabiliana na changamoto hizo kuwa wizara inakamilisha uchambuzi wa taarifa mbalimbali za kisekta ili kubaini kiwango cha athari zitokanazo na mlipuko wa corona katika uchumi na kuainisha mikakati ya muda mfupi, wa kati na mrefu ya kukabiliana nazo.
Mikakati mingine ni, kutunga sera na mkakati wa ufuatiliaji na tathmini ya
miradi na programu za maendeleo na kujenga uwezo wa wataalam wa ndani katika kubuni, kuunda na kuhuisha teknolojia ya mifumo ya usimamizi na ukusanyaji wa mapato.
“Kuhamasisha wadau wa ndani kuendelea kushiriki katika minada ya dhamana za Serikali pamoja na kutafuta vyanzo vingine vya mikopo ya nje vyenye riba nafuu,” amesema Dk. Mpango
Leave a comment