ANGELINA Mabula, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi, amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kwimba, Pendo Malabeja, kuwachukulia hatua watumishi wote wanane wa idara ya ardhi ikiwemo kuwasimamisha kazi kwa kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo, anaandika Moses Mseti
Watumishi hao wanatuhumiwa kutekeleza chini ya kiwango majukumu yao pamoja na kushindwa kuviinguza viwanja 1035 kati ya viwanja 2597 kwenye mfumo wa ulipaji wa kodi kitendo ambacho kimesababisha ukusanyaji wa kodi wilayani humo kusuasua.
Viwanja ambavyo vimeingizwa kwenye mfumo wa ulipaji wa kodi kwa kipindi cha mwaka 2016-2917 ni viwanja 1562 huku wilaya hiyo ikikusanya Sh. Milioni 90 ya kodi ya ardhi wakati lengo ni kukupata Sh. 100 milioni.
Agizo hilo amelitoa wakati akizungumza na watumishi wa idara hiyo pamoja na viongozi mbalimbali akiwemo Mbunge wa Kwimba, Shanif Mansoor, kuhusu utendaji kazi wa idara hiyo ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kikazi ya siku tano mkoani Mwanza.
Mabula amesema kuwa, watumishi wote wa idara hiyo, wanapaswa kuondolewa na kuchukuliwa hatua kwa kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kusababisha halmashauri hiyo kuendelea kudai kiasi cha Sh. Milioni 694 ikiwa ni fedha za kodi ya viwanja.
Mabula amesema kuwa watumishi hao awali walikuwa wakitumia kigezo cha mfumo wa kuingiza rekodi za viwanja kwa kudai mfumo huo upo taratibu (slow) lakini pamoja na mabadiliko hayo bado idadi ya uingizaji wa viwanja haijabadilika kitendo ambacho alimtaka mkurugenzi huyo kuwachukulia hatua.
Amesema kuwa utendaji mbovu wa watumishi hao, unachangiwa na mkurugenzi huyo kushindwa kuwa msimamizi nzuri wa idara hiyo na badala yake yeye amekuwa akiwachekea na badala yake wanaendelea kufanya kazi kwa mazoea.
“Mkurugenzi hapa Kwimba hatuna watumishi wa idara hii ya ardhi, andika barua ya kuomba watu wengine hawa hatuwataki, waende sehemu nyingine na wao wanaendelea kula hela bure, lakini hakuna kazi wanayoifanya na bila posho hawatoki ofisini na kazi yao ni nje.
“Mfumo huu wa kuingiza rekodi ya viwanja ni wa miaka mitatu, kwa muda wote huo hata asilimia 50 hawajaingiza tu, wanafanya kazi kimazoea na hatuwezi kuendelea kufanya kazi na watu goigoi, nikija hapa natoa maelekezo nikiwapa kisogo hakuna mnachokifanya,” amesema Mabula.
Mabula ambaye pia ni Mbunge wa Ilemela mkoani Mwanza amemtaka mkurugenzi huyo kuwachukulia hatua watumishi hao haraka iwezekanavyo na kwamba kama hatafanya hivyo atawaandikia taarifa mbovu kuhusu utendaji wao wa kazi.
Amesema wilaya hiyo ni ya mwisho katika ukusanyaji wa kodi ya ardhi, kutokana na utendaji mbovu wa watumishi hao huku akimtaka na mkuu wa wilaya hiyo na yeye kusimamia suala hilo.
Kwa upande wake mkurugenzi huyo, amesema watalitekeleza agizo hilo kwa mjibu wa taratibu za utumishi wa umma unavyoelekeza licha ya awali kuwatetea watumishi hao kwamba wanashindwa kutekeleza kwa kuwa ni wachache.
Mhandisi Mtemi Msafiri, Mkuu wa wilaya hiyo, awali akisoma taarifa kwa Naibu waziri huyo, alidai watumishi wa wilaya yake, wamebaki watu wakichukua mishahara na kukaa ofisini bila kutekeleza majukumu yao.
“Idara hii ni shida wao mpaka wapewe posho ndiyo watoke ofisini ili waende eneo la tukio na watu wamekuwa wakija hapa wanalipia fedha kwa ajili ya kupimiwa maeneo yao lakini kazi hiyo haifanyiki, hawa wote watafute sehemu nyingine ya kwenda,” amesema Mhandisi Msafiri.
Hata hivyo, amesema hata ripoti aliyoisoma kwa Mabula, aliikataa kutokana na udanganyifu walioufanya na ilikuwa mezani kwake huku akidai baadhi ya watu wamelipa fedha zaidi ya miaka miwili hawajapimiwa maeneo yao kwa uzembe wa watumishi hao.
Mmoja wa wananchi waliofika katika ofisi za mkurugenzi huyo ili kuonana na naibu waziri huyo, Ester James, amesema watumishi hao wanatetewa na mkurugenzi huyo kutokana na malalamiko yao ikiwemo ya kupimiwa maeneo yao kushughulikiwa kwa muda mrefu sasa.
Leave a comment